Friday, June 24, 2016


MANISPAA YA DODOMA YAPOKEA 'CONTAINERS' 60 ZA KUTUNZIA TAKATAKA ZITAKAZOSAMBAZWA KATIKA MITAA MBALIMBALI IKIWA NI HATUA MUHIMU YA KUUWEKA MJI KATIKA HALI YA USAFI ZAIDI. VIFAA HIVYO NI SEHEMU YA UTAKELEZAJI WA MRADI WA KUBORESHA MIJI TANZANIA UNAOFADHILIWA NA BENKI YA DUNIA










Tuesday, June 21, 2016

MADAWATI DODOMA KUKAMILIKA HIVI KARIBUNI NA KUFIKIA MAHITAJI


Mafundi wa madawati kwa ajili ya shule za Manispaa ya Dodoma wakiwa katika eneo lao la kazi ndani ya karakana ya Mhandisi wa Ujenzi

MAADHIMISHO SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI; DODOMA WAASWA KUTUNZA VYANZO VYA MAJI



WANANCHI wanaoishi katika maeneo yenye vyanzo vya maji ikiwemo mabwawa katika Manispaa ya Dodoma wametakiwa kuyalinda na kuyatunza maeneo hayo ili yawe endelevu na kutumiwa na vizazi vya sasa na vijavyo.

Rai hiyo imetolewa na Mstahiki Meya wa Manispaa ya Dodoma Jaffar Mwanyemba wakati alipotembelea bwawa la Matumburu lililopo katika kijiji cha Matumburu Kata ya Matumburu Manispaa ya Dodoma wakati wa maadhimisho ya kilele cha siku ya mazingira duniani inayoadhimishwa Juni tano kila mwaka.

Maadhimisho hayo yaliyofanyika katika kata hiyo kwa ngazi ya Wilaya ya Dodoma yalienda sambamba na zoezi la upandaji wa miti kuzunguka bwawa la Matumburu ili kuboresha mazingira yake na kutunza chanzo hicho muhimu kinachotegemewa na wananchi zaidi ya 9,000 wa kata hiyo na maeneo ya jirani kwa matumizi yao ya kila siku.

Akizungumza na wakazi wa kata hiyo, Mstahiki Meya amewataka wakazi wa Dodoma kutambua umuhimu wa vyanzo hivyo vya maji kwa kuzingatia kuwa mkoa wa Dodoma unapata mvua kidogo katika kipindi cha mwaka mzima.

“Ndugu zangu sisi hapa Dodoma tunapata mvua kidogo sana tena ndani ya kipindi kifupi katika mwaka..ni juzi tu tulikuwa na mafuriko katika baadhi ya maeneo ikiwemo kata hii ya Mpuguzi lakini leo ni pakavu utadhani hapakuwa na mafuriko” alisema.

Katika maadhimisho hayo yaliyochagizwa na kaulimbiu isemayo “Tunza vyanzo vya maji kwa uhai wa Taifa letu”, wadau mbalimbali wa utunzaji wa mazingira walipatiwa vyeti vya kutambuliwa ikiwa ni pamoja na taasisi za elimu kama Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Chuo cha Mipango, na Cho cha Mtakatifu John vilivyopo Manispaa ya Dodoma.
Diwani wa kata ya Mpunguzi John Matonya (kulia) akitoa maelezo kuhusu bwawa la Matumburu lililopo katika kata yake ambapo takribani wakazi 9,000 wanategemea maji ya bwawa hilo kwa matumizi mbalimbali
                                   Shughuli ya maadhimisho ya siku ya Mazingira ikiendelea
 Mstahiki Meya wa Manispaa ya Dodoma Jaffar Mwanyemba akipanda mti katika hifadhi ya bwawa la Matumburu kata ya Mpunguzi jana ikiwa ni maadhimisho ya siku ya mazingira duniani. Takribani wakazi 9,000 wa kata hiyo na maeneo ya jirani wanategemea maji ya bwawa hilo kwa matumizi mbalimbali.

 Wadau mbalimbali wa mazingira wakiwa katika zoezi la upandaji miti katika hifadhi ya bwawa la Matumburu Manispaa ya Dodoma jana.
Naibu Meya wa Manispaa ya Dodoma Jumanne Ngede akipanda mti katika hifadhi ya bwawa la Matumburu kata ya Mpunguzi jana ikiwa ni maadhimisho ya siku ya mazingira duniani. Picha zote: Ramadhani Juma-Ofisi ya Mkurugenzi Manispaa ya Dodoma