Saturday, April 28, 2018

MADIWANI MWANZA WAWEKA HISTORIA JIJINI DODOMA

Diwani wa Kata ya Nyamagana Jijini Mwanza ambaye pia ni Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji hilo Mhe. Bhiku Kotecha (wa pili kushoto-mbele) akiwa na baadhi ya Madiwani na Wataalam wa Halmashauri hiyo walipotembelea Dampo la kisasa la kuhifadhia takataka lililopo eneo la Chidaya Jijini Dodoma jana. Mbele kushoto ni Mhandisi wa Mazingira wa Jiji la Dodoma Barnabas Faida na kulia ni Afisa Habari wa Jiji la Mwanza Martin Sawema. PICHA:DCC
Mhandisi wa Mazingira wa Jiji la Dodoma Barnabas Faida na (kuhoto) akitoa maelezo kuhusu mradi wa Dampo la kisasa la Chidaya kwa Madiwani na Wataalam wa Jiji la Mwanza waliotembelea eneo hilo jana Aprili 27, 2018 kwa lengo la kujifunza. 


Operesheni za kuhifadhi takataka zikiendelea katika Dampo la kisasa la Chidaya Jijini Dodoma.
Mhandisi wa Mazingira wa Jiji la Dodoma Barnabas Faida na (kuhoto) akifuatilia  maswali kuhusu mradi wa Dampo la kisasa la Chidaya kutoka kwa Madiwani na Wataalam wa Jiji la Mwanza waliotembelea eneo hilo jana Aprili 27, 2018 kwa lengo la kujifunza. 
Muonekano wa sehemu ya Dampo la kisasa la Chidaya Jijini Dodoma ambayo bado haijaanza kutumika.


................................................................
MADIWANI wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza wameingia kwenye historia ya kuwa wageni wa kwanza kufanya ziara ya kubadilishana uzoefu katika Halmashauri ya Jiji jipya la Dodoma mara baada ya iliyokuwa Manispaa ya Dodoma kupandishwa hadhi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Magufuli wakati wa Sherehe za miaka 54 ya Muungano Aprili 26, mwaka huu zilizofanyika katika uwanja ya Jamhuri Jijini humo.

Madiwani hao wa jiji la Mwanza wakiongozwa na Naibu Meya Mhe. Bhiku Kotecha ambaye ni Diwani wa Kata ya Nyamagana, walitembelea Halmashauri ya Jiji la Dodoma jana Aprili 27, 2018 ikiwa ni siku moja tangu iliyokuwa Manispaa ya Dodoma kupewa hadhi ya Jiji.

Lengo la ziara hiyo ilikuwa ni kubadilishana uzoefu hususan katika suala la Usafi wa Mazingira, ambapo walitembelea Dampo la kisasa la kuhifadhia takataka kwa njia ya kuzifukia (Sanitary Land Fill) lililopo eneo la Chidaya Kata ya Matumbulu nje kidogo ya Jiji la Dodoma.

Wakiwa katika eneo la Dampo, walipata maelezo ya kina juu ya mradi huo kutoka kwa Mhandisi wa Mazingira wa Jiji la Dodoma Barnabas Faida, ambaye aliwaeleza kuwa, mradi huo umetekelezwa kwa awamu kuanzia mwaka 2011 kwa Fedha za Serikali Kuu ikiwa ni mkopo wa Benki ya Duniani kupitia mradi wa kuimarisha Majiji ya Kimkakati (TSCP) na kwamba hadi kukamilika kwake umegharimu zaidi ya Shilingi Bilioni 7.1, huku ukiwa tayari umeanza kufanya kazi.


Monday, April 23, 2018

KAZI YA UUZAJI WA VIWANJA 10,864 YAZIDI KUSHIKA KASI


Wateja wakieleweshwa eneo vilipo viwanja
Wateja wakiwa katika eneo maalum la kupumzikia wakati wakiendelea na taratibu za ununuzi wa viwanja

Mkuu wa Idara ya Ardhi Mipango Miji na Maliasili Joseph Mafuru (katikati) akishughulikia changamoto ya mteja.

..........................................
KAZI ya uuzaji wa Viwanja 10,684 imeendelea leo Jumatatu Aprili 23, 2018 katika eneo la Ofisi Kuu ya zamani ya Manispaa zilizopo jirani na Sabasaba.

Zoezi hilo lilianza siku ya Ijumaa Aprili 20, 2018, ambapo jumla ya wateja 399 walipatiwa Viwanja kwa ajili ya matumizi mbalimbali.

Katika awamu ya kwanza leo, wateja wapatao 400 wanaotarajiwa kuhudumiwa wamepatiwa kuponi za namba ikiwa ni sehemu ya utaratibu wa kuhudumiwa.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Idara ya Ardhi Mipango Miji na Maliasili Joseph Mafuru, zoezi la uuzaji wa Viwanja litaendelea mpaka Viwanja vyote vitakapomalizika na kwamba Wananchi wote wanakaribishwa.

Saturday, April 21, 2018

MANISPAA YA DODOMA YA PILI NCHINI KWA KUKUSANYA MAPATO

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi akizungumza wakati ukiwasilisha taarifa ya Mikakati na Mipango mbalimbali ya Maendeleo inayotarajiwa kutekelezwa na Manispaa hiyo mbele ya Kamati ya Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Dodoma jana.
Wajumbe wakifuatilia uwasilishaji wa Taarifa.


Wajumbe waalikwa wakifuatilia uwasilishaji wa Taarifa.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi akizungumza wakati ukiwasilisha taarifa ya Mikakati na Mipango mbalimbali ya Maendeleo inayotarajiwa kutekelezwa na Manispaa hiyo mbele ya Kamati ya Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Dodoma jana.

Wajumbe wakifuatilia uwasilishaji wa Taarifa.
Baadhi ya Wataalamu wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma wakifuatilia Mkutano wa Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Dodoma uliopokea taarifa ya Utekeleza wa Ilani ya CCM kuanzia 2015 hadi 2017.

..................................................

HALMASHAURI ya Manispaa ya Dodoma inatarajia kukusanya zaidi ya Shilingi bilioni 67.1 kutoka katika vyanzo vyake vya ndani vya mapato katika mwaka ujao wa Fedha.
Kati ya Fedha hizo, zaidi ya Shilingi bilioni 54.5 sawa na asilimia 81 zitaelekezwa kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo ya Wananchi.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi wa Manispaa hiyo Godwin Kunambi wakati ukiwasilisha taarifa ya Mikakati na Mipango mbalimbali ya Maendeleo inayotarajiwa kutekelezwa na Manispaa hiyo mbele ya Kamati ya Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Dodoma jana.

Kikao hicho kilichofanyika katika Ofisi Kuu ya CCM Taifa Mjini Dodoma, kilikuwa maalum kwa ajili ya wajumbe kupokea taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM kuanzia mwaka 2015 hadi 2017, ambayo awali iliwasilishwa na Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi Kunambi aliwaambia wajumbe wakiongozwa na Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya hiyo Robert Mwinje kuwa, endapo Manispaa ya Dodoma itafanikiwa kufikia lengo hilo la makusanyo, itakuwa ni Halmashauri ya pili Nchini Tanzania kwa kukusanya Fedha nyingi kutoka katika vyanzo vya ndani ikitanguliwa na Manispaa ya Ilala.

Alisema hatua hiyo itaifanya Manispaa ya Dodoma kujiongezea uwezo mkubwa wa kujitegemea ikiwa ni pamoja na kutekeleza miradi ya maendeleo kwa kasi zaidi.

Aliema kuwa, katika kuimarisha ukusanyaji, baadhi ya mikakati itatiliwa mkazo zaidi ikiwemo matumizi ya vifaa na mifumo ya Kielektroniki katika kukusanya, kuwa na takwimu sahihi, usimamizi wa karibu kwa kila chanzo, uibuaji wa vyanzo vipya vya mapato, na kufanya tathimini za mara kwa mara.

Monday, April 16, 2018

ZAIDI YA VIWANJA ELFU KUMI VYAINGIA SOKONI DODOMA




...............................................................
HALMASHAURI ya Manispaa ya Dodoma inatarajia kuuza Viwanja 10,864 kwa ajili ya matumizi mbalimbali ikiwemo Makazi, Biashara, Makazi na Biashara, Taasisi na Viwanda.
 Akiongea na Waandishi wa Habari Mjini Dodoma mwishoni mwa wiki, Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Godwin Kunambi amesema kuwa, Viwanja hivyo vipo katika maeneo ya  Mtumba na Iyumbu kando ya barabara kuu ya Dodoma - Dar es Salaam.
Amesema Viwanja hivyo vitaanza kuuzwa siku ya Ijumaa Aprili 20, 2018 kuanzia saa 2:00 asubuhi katika eneo la Ofisi za Manispaa (Ofisi kuu ya zamani ya Manispaa) zilizopo jirani na Sabasaba.

KWA TAARIFA YA KINA SOMA HAPA CHINI;
Bei za Viwanja zitakuwa kama ifuatavyo kwa mita moja ya mraba:
ENEO LA MTUMBA
UKANDA WA BARABARA YA LAMI
  • Makazi                          8,000/=
  • Makazi na Biashara      8,500/=
  • Biashara                     10,000/=
  • Taasisi                          7,000/=
  • Viwanda vidogo          20,000/=
UKANDA WA KATI
  • Makazi                          6,000/=
  • Makazi na Biashara      7,500/=
  • Biashara                       8,000/=
  • Taasisi                          5,000/=
  • Viwanda vidogo          15,000/=
UKANDA WA BARABARA YA KIKOMBO
  • Makazi                         3,000/=
  • Makazi na Biashara     5,500/=
  • Biashara                      6,000/=
  • Taasisi                         5,000/=
  • Viwanda vidogo         10,000/=
ENEO LA IYUMBU
  • Makazi                         6,000/=
  • Makazi na Biashara     8,000/=
  • Biashara                    15,000/=
  • Taasisi                         7,000/=
  • Viwanda vidogo         20,000/=
Mauzo ya Viwanja yatafanyika kuanzia Ijumaa ya tarehe 20/04/2018. Utaratibu wa mauzo utakuwa kama ifuatavyo:
Kwa wananchi walioomba viwanja Manispaa watafika kwenye eneo la ofisi za zamani za Halmashauri na kuhakiki majina yao ambayo yatakuwa yamebandikwa kwenye mbao za matangazo. Ni lazima mwananchi afike na kitambulisho cha kumtambulisha. Kabla ya kuchagua kiwanja mwananchi anatakiwa kulipa Tshs. 20,000/= za fomu.
Mwananchi akishachagua kiwanja atapewa hati ya madai ya kiwanja hicho na kutakiwa kulipa fedha zote ndani ya siku Thelathini (30) tangu tarehe aliyopokea hati ya madai.
Kwa watumishi wa Umma wanaohamia Dodoma watapelekewa hati ya madai kupitia Makatibu Wakuu wa Wizara zao na watatakiwa kufanya malipo ndani ya siku Thelathini (30).

Wednesday, April 11, 2018

MANISPAA YAZIDI KUING’ARISHA MAKAO MAKUU


Mkuu wa Idara ya Mazingira na Udhibiti wa Taka Ngumu wa Manispaa ya Dodoma Dickson Kimaro akikagua moja ya vifaa vipya vilivyowekwa katika Mtaa wa Kuu kwa ajili kutunza uchafu ikiwa ni juhudi za Manispaa hiyo kuhakikisha Mji unakuwa safi wakati wote.

Mkuu wa Idara ya Mazingira na Udhibiti wa Taka Ngumu wa Manispaa ya Dodoma Dickson Kimaro (kulia) akisimamia uwekaji wa vifaa vipya vya kutunzia uchafu ikiwa ni juhudi za Manispaa hiyo kuhakikisha Mji unakuwa safi wakati wote. Kushoto ni Afisa Mazingira Ally Mfinanga.



Moja ya vifaa vya kutunzia taka kilichopo mkabala na Viwanja vya Nyerere katikati ya Mji.

..................................................

HALMASHAURI ya Manispaa ya Dodoma kupitia Idara ya Mazingira na Udhibiti wa Taka Ngumu imeendelea kuimarisha miundombinu ya usafi kwa kuongeza vifaa vya  kutunza uchafu katika mitaa kadhaa ya Mji ili kuhakikisha Wananchi hawatupi taka ovyo wanapokuwa katika shughuli zao za kila siku.

Akizungumza wakati wa uwekji wa vifaa hivyo, Mkuu wa Idara hiyo Dickson Kimaro alisema Manispaa inatarajia  kuongeza  ‘vitunza uchafu’ 11 katika mitaa mbalimbali ili kuweka mazingira rafiki ya kutunza uchafu kwa Wakazi wa Mji wanaokuwa katika shughuli zao za kila siku.

“Hizi ni juhudi za makusudi ili kuhakikisha Mji wetu unakuwa safi muda wote…natoa wito kwa Wakazi wa Manispaa yetu watumie vifaa hivi kuhifadhia uchafu mdogo wanapokuwa katika shughuli zao za kila siku” alisema Kimaro.

Alisema mbali na vifaa hivyo, tayari Manispaa ilishasambaza vifaa vikubwa vya kukusanyia taka za aina zote (Skip Bucket) 61 katika Kata mbalimbali zinazotumika kama vituo vya kukusanyia taka kabla ya kubebwa na Mitambo ya Manispaa na kupelekwa katika Dampo la Kisasa lililopo eneo la Chidaya Kata ya Matumbulu nje kidogo ya Mji.

Wednesday, April 4, 2018

MILIONI 993 ZA ‘P4R’ ZAIMARISHA ELIMU YA MSINGI

HALMASHAURI ya Manispaa ya Dodoma imeishukuru Serikali kupitia Wizara ya Elimu kwa kuipatia fedha kwa ajili ya kuimarisha Miundombinu ya Shule mbalimbali za Manispaa hiyo chini ya mradi wa ‘Lipa kwa Matokeo’ maarufu kama ‘P4R’.

Shukrani hizo zimetolewa na Afisa Elimu ya Msingi wa Manispaa ya Dodoma Mwisungi Kigosi alipotembelea Shule mbili za Nkuhungu na Chango’mbe ambazo kila moja inajengewa madarasa mapya nane kwa fedha za mradi huo.

Kwa mujibu wa Kigosi, mradi huo pamoja na mambo mengine, unajenga miundombinu mbalimbali katika Shule sita za Msingi ambapo jumla ya Shilingi milioni 993.1 zinatekeleza kazi hizo.

“Fedha za P4R zina kazi nyingi kama vile kusaidia kukusanya takwimu mbalimbali, kuhamisha Walimu kwa mujibu wa Ikama, na kubwa kabisa ni kujenga miundombinu kama madarasa mapya, kukarabati madarasa ya zamani, na kujenga Vyoo” Alifafanua.

Alisema mradi huo umekuwa mkombozi kwa Shule husika kwa kuongeza na kuimarisha miundombinu kama madarasa kutokana na idadi kubwa ya Wanafunzi inayopelekea upungufu wa madarasa katika baadhi ya Shule.

“Kwa mfano Shule ya Msingi Nkuhungu, mwaka huu wanafunzi walioandikishwa kuanza darasa la kwanza ni mia sita…kwa hiyo utaona ni jinsi gani madarasa yanahitajika na hii inatokana na Kata hiyo kuwa na Shule  moja tu ya Serikali” alisema Kigosi.

Aidha, alizitaja Shule nyingine nne ambako mradi huo unatekelezwa kuwa ni Mahomanyika, Mwenge, Ihumwa, na Nzasa, na kwamba Fedha hizo zimepatikana baada ya Manispaa kukidhi vigezo ikiwemo kuwa na takwimu za uhakika za masuala ya Elimu.

Baadhi ya Wanafunzi wa Shule zilizopata Fedha za mradi huo wamepongeza juhudi za Serikali katika kuwatatulia chang’amoto hususani za miundombinu kama vyumba vya Madarasa na Vyoo.

Mkuu wa Idara ya Elimu Msingi katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Mwisungi Kigosi akizungumza na Dada Mkuu wa Shule ya Msingi Nkuhungu Zena Yusuph alipotembelea Shule hiyo jana kukagua Maendeleo ya Ujenzi wa Miundombinu ikiwemo Vyumba vya Madarasa kupitia mradi wa 'P4R'. Wanafunzi wa Darasa la Saba na la nne katika Shule hiyo wanaendelea na masomo ili kujiimarisha zaidi kuelekea mitihani ya Kitaifa mwishoni mwa Mwaka huu.
Mkuu wa Idara ya Elimu Msingi katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Mwisungi Kigosi (kulia) akikagua Maendeleo ya Ujenzi wa Madarsa nane alipotembelea Shule ya Msingi Nkuhungu  jana kukagua Maendeleo ya Ujenzi wa Miundombinu ikiwemo Vyumba vya Madarasa kupitia mradi wa 'P4R'. Kushoto ni Msimamizi wa Ujenzi kutoka Suma JKT Joseph Luya.
Moja ya jengo lenye Vyumba vya Madarasa yaliyojengwa kupitia mradi wa P4R katika Shule ya Msingi Chang'ombe. Jumla ya Vyumba vipya nane vya Madarasa vimejengwa katika Shule hiyo.
Mkuu wa Idara ya Elimu Msingi katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Mwisungi Kigosi akizungumza na baadhi ya Wanafunzi wa Shule ya Msingi Nkuhungu alipotembelea Shule hiyo jana kukagua Maendeleo ya Ujenzi wa Miundombinu ikiwemo Vyumba vya Madarasa kupitia mradi wa 'P4R'. Wanafunzi wa Darasa la Saba na la nne katika Shule hiyo wanaendelea na masomo ili kujiimarisha zaidi kuelekea mitihani ya Kitaifa mwishoni mwa Mwaka huu.
Moja ya jengo lenye Vyumba vya Madarasa yaliyojengwa kupitia mradi wa P4R katika Shule ya Msingi Nkhungu. Jumla ya Vyumba vipya nane vya Madarasa na matundu matano ya Vyoo vimejengwa katika Shule hiyo.

KITUO CHA DALADALA JAMATINI KUENDELEA KUTUMIKA, MABASI YA MIKOANI YAONYWA


Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Binilith Mahenge akizungumza na wadau wa usafishaji katika Stendi Kuu ya muda Mabasi ya Mikoani iliyopo eneo la Nanenane jana Aprili 3, 2018 alipofanya ziara fupi katika stendi hiyo.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi akifafanua jambo wakati Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Binilith Mahenge alipozungumza na wadau wa usafishaji katika Stendi Kuu ya muda ya Mabasi ya Mikoani iliyopo eneo la Nanenane jana Aprili 3, 2018 alipofanya ziara fupi katika stendi hiyo.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (katikati) akifafanua jambo wakati Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Binilith Mahenge (kushoto) alipofanya ziara fupi kukagua maeneo yanayoweza kuwekewa miundombinu muhimu na kutumika kama kituo cha daladala cha Mjini,  jana Aprili 3, 2018.

........................................
MKUU wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Binilith Mahenge ameelekeza matumizi ya kilichokuwa kituo Kikuu cha Mabasi madogo maarufu kama Daladala cha Jamatini Mjini Dodoma kwa ajili ya kupakia na kushusha abiria wanaotoka katika maeneo mbalimbali ya Manispaa hiyo yaendelee kama kawaida wakati Manispaa ikiandaa eneo mbadala.

Mkuu huyo wa Mkoa pia ameagiza ‘ruti’ za Daladala zifupishwe kama ilivyokuwa awali, na kwamba upangaji wa ‘ruti’ ndefu ujadiliwe upya na wadau wote wanaohusika na endapo utakubaliwa na wengi ndipo utekelezaji wake uanze.

Dokta Mahenge ametoa maelekezo hayo leo Aprili 3, 2018, alipokuwa akizungumza na wadau wa usafirishaji katika kituo kikuu cha mabasi ya Mikoani cha muda kilichopo Nanenane Manispaa ya Dodoma baada ya kituo hicho kufungwa wiki iliyopita kwa ajili ya kupisha mradi wa Reli ya Kisasa.

Hatua hiyo imefikiwa baada ya majadiliano na wadau wote ikiwemo Mamlaka ya Usimamizi wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMTRA), Manispaa, Jeshi la Polisi, na Shirika la Reli ambao ndio wamiliki wa eneo hilo, na kwamba matumizi ya stendi hiyo yataendelea kwa muda wa miezi miwili kuanzia sasa, kipindi ambacho Manispaa itatakiwa kuwa imeshapata na kuandaa stendi mbadala.

Akizungumza katika eneo la tukio, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi alisema Manispaa imepokea maagizo yote na itahakikisha inaandaa eneo kwa ajili ya Stendi ya Mabasi madogo Mjini katika kipindi cha miezi miwili kama ilivyoelekezwa na Mkuu wa Mkoa.

Katika hatua nyingine, Mkuu huyo wa Mkoa ameagiza mabasi yote yanayosafirisha abiria Mikoa mbalimbali Nchini kupakia na kuanzia safari zao katika kituo Kikuu cha mabasi ya muda kilichopo Nanenane na Kampuni itakayokiuka itachukuliwa hatua kali za Kisheria.

“Namuagiza Mkuu wa Jeshi la Polisi kikosi cha Usalama Barabarani wa Mkoa kuwa, kuanzia kesho mabasi yote yauze tiketi na kuanza safari zao hapa katika kituo hiki Kikuu cha mabasi cha muda cha Nanenane…hakuna Mkubwa wala mdogo katika kutoa huduma kwa Wananchi” alisisitiza Dkt. Mahenge.