Wednesday, May 30, 2018

JIJI LA DODOMA VINARA UMISETA


Mkuu wa Idara ya Elimu Sekondari wa Jiji la Dodoma Mwalimu Abdallah Membe akionesha kikombe cha ubingwa wa Michezo ya UMISETA Kimkoa iliyofanyika kwa siku tatu katika Viwanja vya Sekondari ya Dodoma kuanzia Mei 26 mwaka huu. 
Mkuu wa Idara ya Elimu Sekondari wa Jiji la Dodoma Mwalimu Abdallah Membe akipokea kikombe cha ubingwa wa Michezo ya UMISETA Kimkoa iliyofanyika kwa siku tatu katika Viwanja vya Sekondari ya Dodoma kuanzia Mei 26 mwaka huu. 
Washiriki wakiwa wameketi kando ya vikombe vilivyotolewa kwa washindi


..................................................

HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imeibuka mshindi wa jumla baada ya kushinda michezo mingi katika michezo ya Shule za Sekondari (UMISETA) iliyofanyika kwa siku tatu kuanzi Mei 26, 2018 na kushirikisha zaidi ya Wanamichezo 700 kutoka katika Wilaya zote za Mkoa wa Dodoma, huku Wilaya ya Kongwa ikishika nafasi ya pili na Mpwapwa nafasi ya tatu.

Timu ya Wanamichezo wa Jiji la Dodoma iliibuka bingwa wa Mkoa baada ya kushinda michezo ya Mpira wa Mikoni kwa Wavulana, Mpira wa Pete, Mpira wa Miguu kwa Wasichana, Kikapu kwa Wavulana na Wasichana, kurusha tufe, kurusha kisahani,
na riadha kwa mita 200.

Mkuu wa Idara ya Elimu Sekondari wa Jiji la Dodoma Mwalimu Abdallah Membe amesema amefurahishwa na ushindi walioupata na kwamba wao kama Jiji walijipanga vizuri, huku akiwapongeza wote waliofanikisha mafanikio hayo wakiwemo Wanafunzi, Walimu, na wadau wengine wote.

Amesema baada ya hatua hiyo kufikia tamati, timu ya Mkoa ya Michezo hiyo itasafiri Jumapili wiki hii kuelekea Jijini Mwanza kushiriki michezo hiyo kwa ngazi ya Taifa inayotarajiwa kuanza Jumatatu Mei 4 mwaka huu Jijini humo.


Saturday, May 26, 2018

WAZIRI JAFFO: JIJI LA DODOMA NI MFANO NCHINI KUWATAMBUA WAZEE


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali (TAMISEMI) Selemani Jaffo akimkabidhi kitambulisho rasmi cha kumtambua mmoja ya Wazee wa Kata ya Mkonze Halmashauri ya Jiji la Dodoma wakati Waziri huyo alipozindua zoezi hilo mapema leo Mei 26, 2018. Wanaoshudia ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi (kulia kwa Waziri) na Mkurugenzi wa Jiji hilo Godwin Kunambi (mwenye shati jeupe). Kushoto kwa Waziri aliyevaa miwani ni Mganga Mkuu wa Jiji la Dodoma Hamadi Nyembea.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali (TAMISEMI) Selemani Jaffo (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na badhi ya Waze wa Kata ya Mkonze Jijini Dodoma baada ya kuzindua na kuwakabidhi vitambulisho rasmi vya kuwatambua  Wazee katika Halmashauri ya Jiji hilo mapema leo Mei 26, 2018. Kulia ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi na kushoto ni Mkurugenzi wa Jiji hilo Godwin Kunambi (mwenye shati jeupe). 
Baadhi ya Wazee wa Kata ya Mkonze Jijini Dodoma wakifuatilia hafla ya uzinduzi wa utaoji wa vitambulisho vya Wazee uliofanywa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI Selemani Jaffo leo Mei 26, 2018.
Diwani wa Kata ya Mkonze Jiji la Dodoma David Bochela akitoa neno wakati wa hafla ya uzinduzi wa utaoji wa vitambulisho vya Wazee uliofanywa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI Selemani Jaffo leo Mei 26, 2018 katika Kata hiyo.

...........................................................................


WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Selemani Jaffo amesema, Halmashauri ya Jiji la Dodoma ni ya mfano Nchini katika kuwatambua na kuwatengenezea vitambulisho maalum vya kuwatambulisha Wazee katika maeneo ya huduma mbalimbali ikwemo matibabu, akiwa ni utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Wazee ya mwaka 2003 inayolenga katika  kuhakikisha kuwa, Wazee wa Tanzania wanatambuliwa na wanapewa fursa ya kushiriki katika mambo yanayohusu maisha ya kila siku na kupata huduma zote za msingi.

Waziri Jaffo ameyasema hayo mapema leo Mei 26, 2018, alipokuwa akizindua rasmi zoezi la utoaji wa vitambulisho vya Wazee kwenye hafla fupi iliyofanyika katika Kata ya Mkonze iliyopo umbali wa kilometa 4.7 kutoka katikati ya Jiji la Dodoma.

Akizungumza wakati wa  hafla hiyo ambayo pia ilihudhuriwa na Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi na Mkurugenzi wa Jiji hilo Godwin Kunambi, Waziri huyo aliagiza Halmashauri za Mikoa yote 26 ya Tanzania Bara  kuhakikisha zinawatambua Wazee katika maeneo yao na kuwasilisha taarifa kamili ya kila Mkoa kuhusu Wazee katika  Ofisi yake ifikapo Juni 30, mwka huu.

Awali, akiwasilisha taarifa ya utekeleaji wa zoezi hilo kwa niaba ya Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Godwin Kunambi, Mganga Mkuu wa Jiji hilo Hamadi Nyembea alisema Halmashauri ilianza zoezi hilo kwa kuwatambua Wazee katika Kata zote 41 za Jiji la Dodoma, na kwamba mpaka sasa jumla ya Wazee 15, 854 wameshatambuliwa kutoka katika Kata 33, sawa na asilimia 80.5.

Alisema, hatua iliyofuata ni kuwapiga picha Wazee waliotambuliwa na kuwatengenezea vitambulisho, zoezi lililoanza rasmi mwezi Februari Mwaka huu, ambapo jumla ya Wazee 1,118 wameshapigwa picha katika Kata za Mkonze, Mnadani, Uhuru, Madukani, Makole na Majengo na kwamba kazi hiyo inaendelea katika Kata zilizobaki.

“Jumla ya vitambulisho 564 vya Wazee vimeshakamilika na wahusika watakabidhiwa rasmi leo kwa ajili ya kuanza kuvitumia” alisema Mganga Mkuu huyo wakati akiwasilisha taarifa hiyo.


Friday, May 25, 2018

MKURUGENZI JIJI LA DODOMA ATANGAZA NEEMA KWA WATEJA WA VIWANJA


Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Godwin Kunambi (kulia) akizungumza na Waandishi wa Habari leo ambapo ameongeza muda wa wateja wa Viwanja kulipa gharama za Viwanja vyao kutoka Mwezi mmoja wa awali hadi miezi mitatu sasa.
Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Godwin Kunambi (kulia) akizungumza na Waandishi wa Habari leo ambapo ameongeza muda wa wateja wa Viwanja kulipa gharama za Viwanja vyao kutoka Mwezi mmoja wa awali hadi miezi mitatu sasa.

Mtaalamu wa Jiji la Dodoma akimuelekeza mteja kwenye ramani inayoonesha mgawanyo wa Viwanja ili aweze kuchagua kiwanja kwa mujibu wa mahitaji yake katika zoezi la uuzwaji wa Viwanja linaloendelea sasahivi katika Halmashauri ya Jiji hilo.
Ramani ya Tanzania ikionesha Jiji la Dodoma lilipo kutoka katika Mikoa mingine yote ya Tanzania.

..............................................................................


HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imeongeza muda wa kulipia Viwanja kwa wateja wake wote walionunua Viwanja kuanzia Aprili 20, mwaka huu kutoka siku 30 yaani Mwezi mmoja hadi siku 90 yaani miezi mitatu.

Aidha, Halmashauri hiyo inatarajia kuendelea kuuza Viwanja vya eneo la Iyumbu kuanzia tarehe 5 Juni, 2018 kwani tayari imeshamaliza kazi ya kushughulikia malalamiko ya Wakazi wa Ngaloni walioibuka na kudai kutolipwa fidia hapo awali.

Hayo yametangazwa na Mkurugenzi wa Jiji hilo Godwin Kunambi wakati akiongea na Waandishi wa Habari Jijini humo leo ambapo amesema Halmashauri imefikia uamuzi huo baada ya kuridhika na mwenendo wa wateja kulipia Viwanja vyao ambapo mpaka sasa zaidi ya shilingi bilioni 4 zimeshalipwa kwa Wananchi kama fidia ya maeneo yao yaliyotwaliwa wakati wa upimaji.

Alitoa wito kwa wateja wote walionunua viwanja na wanaoendelea kununua kutumia muda ulioongezwa kama fursa ya kukamilisha malipo yao ili kuepuka usumbufu usio wa lazima baada ya muda huo kumalizika.

“Kwa wale wote waliokuwa wanasubiri Viwanja vya Iyumbu wafike katika eneo letu la kuuzia Viwanja ambalo ni Ofisi za Manispaa ya zamani jirani na Sabasaba siku ya tarehe 5 mwezi ujao…tutaanza kuviuza siku hiyo” alisema Kunambi.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi huyo wa Jiji ametoa muda wa miezi mitatu kwa watu wote waliopewa Viwanja na iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) katika maeneo ya Njedengwa, Miganga, Mkonze, Iyumbu New Town Center, na Mkalama na hawajakamilisha malipo ya Viwanja hivyo kukamilisha ndani ya kipindi hicho vinginevyo Halmashauri itavitwaa kwa mujibu wa Sheria na kuviuza kwa wateja wengine wenye mahitaji.  


Thursday, May 24, 2018

‘VITA’ SARATANI YA SHINGO YA KIZAZI YAZINDULIWA DODOMA


Mwanafunzi wa Kidato cha pili katika shule ya Sekondari ya Dodoma Huda Khalid Rabash akionesha kadi yake aliyokabidhiwa na Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi (kushoto) kama ishara ya uzinduzi rasmi wa utoaji wa chanjo ya kinga dhidi ya ugonjwa wa Saratani ya Shingo ya kizazi kwa Wanawake. Kadi hiyo itamuwezesha kupata chanjo hiyo kwa awamu ya pili baada ya miezi sita ili kukamilisha kinga yake dhidi ya ugonjwa huo. Wengine wanaoshuhudia ni Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Hamadi Nyembea (mwenye miwani katikati nyuma)  na Mkuu wa Shule hiyo Mwalimu Amani Mfaume (mwenye miwani katikati mbele). Kushoto ni Mwalimu wa Afya wa Shule hiyo Caritas Burchard. PICHA ZOTE: RAMADHANI JUMA-OFISI YA MKURUGENZI
Muhudumu wa Afya Ruth Azaliwa akimchoma Sindano ya chanjo dhidi ya Saratani ya Shingo ya Kizazi kwa Wanawake Mwanafunzi wa kidato cha pili wa Shule ya Sekondari ya Dodoma Huda Khalid Rabash kuashiria uzinduzi wa zoezi la utoaji wa chanjo hiyo katika Wilaya ya Dodoma jana. Wanaoshuhudia ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi (kushoto) na Mwalimu wa Afya wa Shule hiyo Caritas Burchard (kulia).
Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi akimkabidhi kadi maalum kwa ajili kupata huduma ya chanjo awamu ya pili dhidi ya ugonjwa wa Saratani ya Shingo ya kizazi kwa Wanawake Mwanafunzi wa kidato cha pili wa Shule ya Sekondari ya Dodoma Huda Khalid Rabash kama ishara ya uzinduzi wa zoezi la utoaji wa chanjo hiyo katika Wilaya ya Dodoma jana katika ukumbi wa Shule hiyo.  
Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Hamadi Nyembea akizungumza wakati wa uzinduzi wa zoezi la utoaji wa chanjo dhidi ya ugonjwa wa Saratani ya Shingo ya kizazi kwa Wasichana walio chini ya umri wa miaka 14 katika Wilaya ya Dodoma jana. Katikati ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi na wa kwanza ni Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Dodoma palikofanyika uzinduzi huo Mwalimu Amani Mfaume. 
Sehemu ya Wanafunzi wa kike wa Shule ya Sekondari ya Dodoma wakifuatilia shughuli ya uzinduzi wa utoaji wa chanjo dhidi ya ugonjwa wa Saratani ya Shingo ya Kizazi  uliofanyika katika Shule hiyo jana.
Zoezi la utoaji wa chanjo dhidi ya ugonjwa wa Saratani ya Shingo ya kizazi kwa Wasichana walio chini ya umri wa miaka 14 likiendelea katika Sekondari ya Dodoma mara baada ya kuzinduliwa rasmi na Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi.


................................................

ZOEZI la utoaji wa chanjo ya kinga dhidi ya ugonjwa wa Saratani ya Shingo ya Kizazi kwa Wanawake limezinduliwa rasmi katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma huku wasichana waliopatiwa chanjo hiyo wakitoa wito kwa wenzao kujitokeza na kuhakikisha wanakingwa dhidi ya ugonjwa huo.

Uzinduzi huo umefanyika jana katika ukumbi wa Dodoma Sekondari ambapo mgeni rasmi katika hafla fupi ya uzinduzi huo alikuwa Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi huku Mganga Mkuu wa Halmashauri Hamadi Nyembea akimwakilisha Mkurugenzi Godwin Kunambi.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Kaimu Mkuu huyo wa Wilaya alisema uzinduzi huo ni kiashiria cha kuwafikia Wasichana wote wenye chini ya umri wa miaka 14 ndani ya Wilaya ya Dodoma.
Alisema zoezi hilo litaendeshwa na Halmashauri kupitia Ofisi ya Mganga Mkuu, na litashirikisha viongozi wa ngazi zote ikiwemo Kata na Mitaa ili kuhakikisha kila msichana anayehusika anafikiwa na kupatiwa chanjo hiyo.

Awali, Mganga Mkuu wa Halmashauri Hamadi Nyembea alisema katika kipindi cha Mwaka mmoja ujao, jumla ya Wasichana 7,828 walio na umri wa chini ya miaka 14 wanatarajiwa kufikiwa na kupatiwa chanjo hiyo katika Wilaya ya Dodoma.

Alisema  baada ya miezi sita Wasichana wote waliopatiwa chanjo hiyo watapatiwa tena kwa awamu ya pili ili kukamilisha kinga yao dhidi ya virusi vinavyoeneza ugonjwa huo.

Alimweleza Mgeni rasmi na wajumbe kuwa, chanjo hiyo imethibitishwa na Shirika la AfyaDuniani (WHO) hivyo Wasichana na Wazazi wasiwe na mashaka badala yake watoe ushirikiano wa kutosha ili kufikia lengo la Serikali la kutokomeza ugonjwa huo kama ilivyofanya kwa magonjwa kama Polio.

Tuesday, May 22, 2018

NAIBU WAZIRI LUGOLA APONGEZA UJENZI DAMPO LA KISASA


Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola (mwenye sare ya bluu) akipata maelezo jinsi mzani uliopo katika Dampo la kisasa la kuhifadhia taka lililopo Chidaya Manispaa ya Dodoma unavyofanya kazi kwa njia ya Kompyuta, kutoka kwa Mhandisi wa Mazingira wa Halmashauri hiyo Barnabs Faida.  
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola (mwenye sare ya bluu) akifuatilia maelekezo ya jinsi maabara ya kupima kemikali kwenye maji ya ardhini katika eneo la Dampo la kisasa la Halmashauri ya  Manispaa ya Dodoma inavyofanya kazi ili kuhakikisha nuwepo wa Dampo hilo hauhatarishi vyanzo vya maji katika maeneo ya jirani. Anayetoa maelezo ni Afisa Mazingira kutoka Idara ya Mazingira na Udhibiti wa Taka Ngumu ya Halmashauri hiyo  Happynes Pastory.
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola (wa tatu kushoto) akiwa katika eneo la Dampo la kisasa la kuhifadhia taka lililopo Chidaya Manispaa ya Dodoma alipofanya ziara kukagua Mifumo ya usimamizi wa Mazingira katika Dampo hilo inavyofanya kazi. Wa pili kushoto ni Diwani wa Kata ya Ntyuka Theobald Maina.
Sehemu ya Dampo iliyoanza kutumika
Sehemu ya pili ya Dampo ambayo itatumika baada ya sehemu ya kwanza kujaa

...................................................................

NAIBU Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Kangi Lugola ameipongeza Halmashauri ya Manispaa Dodoma kwa ujenzi wa Dampo la kisasa la kuhifadhia taka kwa teknolojia ya kuzizika ardhini (Sanitary Land Fill) lililopo eneo la Chidaya Kata ya Matumbulu katika Halmashauri hiyo.

Alitoa pongezi hizo jana baada ya kufanya ziara katika Dampo hilo kwa lengo la kukagua mifumo ya usimamizi wa Mazingira.
“Mfikishieni Mkurugenzi wa Halmashauri salamu zangu…nimeridhika na uendeshaji wa Dampo hili na jinsi mnavyozingatia na kusimamia usalama wa Mazingira” alisema Naibu Waziri huyo.

Alisema ni fahari kubwa kwa Halamshauri ya Manispaa ya Dodoma kuwa na Miundombinu ya kisasa ya usafi na kutaka taka zote zinazozalishwa ziondolewe na kupelekwa katika Dampo hilo ili kufiki malengo ya mradi huo.

Dampo hilo lilianza kujengwa mwaka 2010 na hadi linakamilika limegharimu zaidi ya Shilingi bilioni 7.1 ambazo ni mkopo kutoka Benki ya Dunia kupitia Serikali Kuu ikiwa ni utekelezaji wa mradi wa kuendeleza Miji ya Kimkakati Tanzania (TSCP) inayoratibiwa na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).

Naibu Waziri Lugola alikuwa katika siku ya pili ya ziara yake ya siku saba katika Wilaya ya Dodoma ambapo pamoja na mambo mengine, anakagua jinsi mifumo ya usimamizi wa Mazingira katika taasisi mbalimbali ikiwemo Hospitali na Vyuo inavyosimamiwa na kufanya kazi.


Friday, May 18, 2018

WAZIRI LUGOLA AANZA ZIARA YA WIKI MANISPAA YA DODOMA


Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola (wa pili kulia) akikagua mifumo ya usimamizi wa Mazingira katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma jana. Kushoto ni Afisa Mazingira wa Manispaa ya Dodoma Dickson Kimaro na pili kushoto ni Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mzee Nassoro. Wa tatu kutoka kulia ni Afisa Afya wa Mkoa wa Dodoma Carle Lyimo. PICHA ZOTE-RAMADHANI JUMA
Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mzee Nassoro akitoa maelezo kwa Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola (katikati) wakati wa ziara ya kiongozi huyo katika hosptali hiyo jana.
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola (kulia) akikagua mifumo ya usimamizi wa Mazingira katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma jana. Kulia ni Afisa Afya wa Mkoa wa Dodoma Carle Lyimo.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola akiwa katika sehemu ya Vyoo ya moja ya Wodi ya wagonjwa  akikagua mifumo ya usimamizi wa Mazingira katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma jana.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Kangi Lugola (kulia) akihakiki moja ya 'chemba' za mifumo ya maji katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu John wakati alipofanya ziara ya kukagua mifumo ya usimamizi wa Mazingira chuoni hapo jana.



..........................................................................


NAIBU Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Kangi Lugola ameanza ziara ya kikazi ya wiki moja katika Manispaa ya Dodoma jana ambapo alitembelea Ofisi za Halmashauri na kupokea taarifa ya hali ya Mazingira kwa ujumla iliyowasilishwa na Mkuu wa Idara ya Mazingira na udhibiti wa taka ngumu Dickson Kimaro.

Naibu Waziri pia alipata taarifa kutoka kwa wataalam wa taasisi zingine ambazo ni wadau wa Mazingira ikiwemo Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA), Idara ya Madini, na Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) ambao amefutana nao katika ziara hiyo.

Katika siku ya kwanza ya ziara yake hapo jana, Naibu Waziri Lugola alitembelea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma na Chuo Kikuu cha Mtakatifu John ambapo alikagua mifumo ya usimamizi wa taka ambapo kwa ujumla alikiri kuridhishwa jinsi taasisi hizo zinavyozingatia matakwa ya Sheria na taratibu za kuhifadhi Mazingira, lakini aliziagiza kuhakikisha takataka zinazoteketezwa kwa kuchomwa moto zinateketea kwa kiwango kinachokubalika.


Ziara ya Naibu Waziri inaendelea leo Ijumaa Mei 18, 2018 ambapo pamoja na maeneo mengine, atatembelea na kukagua mifumo ya usimamizi wa taka katika machinjio ya Punda iliyopo eneo la Kizota   na inatarajiwa kumalizika Mei 25, mwaka huu.     



Thursday, May 17, 2018

LAAC YA UGANDA ZIARANI DODOMA, YAFURAHIA MJI WA SERIAKLI


Mwakilishi wa Mkuu wa Idara ya Ujenzi wa Manispaa ya Dodoma Mhandisi Emanuel Manyanga akiwasilisha taarifa ya Miradi iliyotekelezwa na itakayotekelezwa kupitia Mradi wa Uendelezaji Miji ya Kimkakati Tanzanzia (TSCP) mbele ya Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Serikali za Mitaa ya Nchini Uganda ilipokuwa katika ziara ya kujifunza katika Manispaa hiyo jana. PICHA: OFISI YA MKURUGENZI
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Serikali za Mitaa ya Nchini Uganda Reagan Okumu (kushoto) akizungumza wakati alipowaongoza wajumbe wa Kamati hiyo katika ziara ya kujifunza katika Manispaa ya Dodoma jana.
Mhandisi wa Mazingira wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Barnabas Faida akitoa neno la utangulizi kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kwa Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Hesbu za Srikali za Mitaa ya Uganda ilipotembelea Halmashauri hiyo jana.
WAJUMBE wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa ya Bunge la Uganda wakifuatilia taarifa za miradi ya Ujenzi iliyokuwa akiwasilishwa na Mhandisi Emanuel Manyanga kutoka Idara ya Ujenzi ya Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma walipofanya ziara ya kujifunza juu ya utekelezaji wa miradi ya Kimkakati. 

............................................................

WAJUMBE wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa ya Bunge la Uganda wameishukuru Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma kwa kuipatia Serikali ya Nchi hiyo kiwanja chenye ukubwa wa eka tano katika Kata ya Mtumba eneo utakapojengwa Mji wa Serikali.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo Reagan Okumu alitoa Shukrani hizo jana wakati Kamati hiyo ilipotembelea Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma walipokuwa katika ziara ya siku moja ya kujifunza mambo mbalimbali ikiwemo utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati kama Dampo la kisasa la kuhifadhia taka kwa kuzifukia ardhini (Sanitary Land Fill) lililopo Kata ya Matumbulu ambalo ni moja ya miradi mikubwa katika eneo la usafi na utunzaji wa mazingira.

Awali akizungumza mbele ya Kamati hiyo, Mhandisi wa Mazingira wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma ambaye alimwakilisha Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Godwin Kunambi, aliwajulisha wajumbe hao kuwa, Halmashauri imetenga na kupima eneo litakalojengwa Mji wa Serikali hapa Dodoma na kwamba Serikali ya Uganda imepewa kiwanja chenye ukubwa wa eka tano kwa ajili ya matumizi ya kiofisi, ambapo pia walioneshwa ramani ya eneo hilo.

Wajumbe wa Kamati hiyo waliezea kufurahishwa kwao na hatua hiyo huku wakiahidi kufikisha taarifa hizo njema kwa Wananchi wa Uganda mara watakaporejea Nchini humo.