Monday, July 30, 2018

JIJI LA DODOMA LATOA MILIONI 950 KWA WANAWAKE NA VIJANA, WAZIRI JAFO AKABIDHI HUNDI





....................................................................

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Selemani Jafo amekabidhi hundi ya Shilingi Milioni 950 zilizotolewa na Halmashauri ya Jiji la Dodoma kutoka katika Mfuko wa Wanawake, Vijana, na Walemavu kwa ajili ya vikundi 234 vya Wanawake na Vijana huku akitoa wito kwa Jiji hilo kutafuta masoko ya bidhaa  zinazozalishwa na vikundi hivyo kwani imekuwa moja ya changamoto zinazowakabili katika shughuli zao.

Hafla ya kukabidhi hundi hiyo kwa Wanavikundi hao imefanyika hivi karibuni katika Viwanja vya Nyerere vilivyopo katikati ya Jiji la Dodoma.

‘’Viongozi muandae Mpango Mkakati wa kuwa na masoko ya kuuza bidhaa za wajasiriamali hawa, nimeona wana bidhaa nzuri sana ambazo unaweza usiamini kama zinatoka Dododma, lakini kila mmoja ukimuuliza soko anakwambia hana soko maalumu’’ Alisema Waziri Jafo.

Aliongeza ‘’Mbali na kuwapa fedha lakini pia nakuagiza Mkurugenzi wa Jiji (Godwin Kunambi ) na Mstahiki Meya (Profesa David Mwamfupe) mtafute eneo la kimkakati kwa ajili ya hawa mnaowapatia mkopo na vikundi vyote vilivyowezeshwa na Halmashauri hii, kwa kufanya hivi tunaweza kuwa na eneo moja maalumu ambalo litakuwa linafanya maonyesho kwa mwaka mzima’’ Alisema.

Awali, Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Godwin Kunambi alimweleza Waziri Jafo kuwa, fedha hizo zinatokana na ukusanyaji bora wa mapato ya ndani na kwamba kwa sasa Halmashauri inatoa mikopo mikubwa kuanzia Shilingi milioni moja hadi milioni kumi na kutoa wito kwa wajasiriamali kujiunga katika vikundi vya kiuchumi ili kukidhi vigezo vya kupata mikopo hiyo.

Alisema fedha hizo zinatolewa kwa vikundi 234 vya Wajasiriamali, vikiwemo 168 vya Wanawake pamoja na vikundi 66 vya Vijana.


Thursday, July 12, 2018

MKATABA WA KIHISTORIA DODOMA YA KIJANI WASAINIWA

Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Godwin Kunambi (kushoto) na Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Professa Dos Santos Silayo wakisaini hati ya makubaliano ya kupanda na kustawisha miti, na kuhifadhi misitu iliyopo ndani ya Jiji la Dodoma kwa lengo la kuikijanisha Dodoma.
Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Godwin Kunambi (kushoto) na Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Huduma za Misitu Tanzania  (TFS) Professa Dos Santos Silayo wakikabidhiana hati ya makubaliano.


Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Godwin Kunambi (kushoto) akifafanua jambo mbele ya Mtendaji Mkuu ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Professa Dos Santos Silayo kuhusu maeneo waliyokubalina kupanda na kustawisha miti, na kuhifadhi misitu iliyopo ndani ya Jiji la Dodoma kwa lengo la kuikijanisha Dodoma. 

........................................................................
HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma na Wakala ya Huduma za Misitu Tanzania (TFS) zimesaini hati ya makubaliano (MOU) ya upandaji, ustawishaji, na utunzaji wa miti na uhifadhi wa misitu iliyopo katika Jiji hilo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Kampeni ya Dodoma ya Kijani iliyozinduliwa rasmi na Makamu wa Rais  Mhe. Samia Saluhu Hassan kwa kupanda miti kwenye eneo la Mzakwe mwishoni mwa mwaka jana.
Hafla ya utiaji saini makubaliano hayo ambayo ni ya kwanza kufanywa na TFS Nchini ilifanyika jana katika Ofisi za Jiji, ambapo Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Godwin Kunambi na Mtendaji Mkuu wa TFS Profesa Dos Santos Silayo walisaini makubaliano hayo ambayo utekelezaji wake unaanza katika mwaka huu wa fedha.
Akizungumza katika hafla hiyo ambayo pia ilihudhuriwa na Waandishi wa Habari wa Vyombo mbalimbali, Mkurugenzi Kunambi alisema Jiji linawakabidhi TFS hekta 150 za msitu katika eneo la Mahomanyika ili kustawisha miti na kulihudumia.
“Lakini pia kwa makubaliano haya, TFS watahifadhi maeneo yote ya vilima vilivyopo ndani ya Jiji la Dodoma na kustawisha misitu midogo katika maeneo ya makazi yaliyotengwa kwa ajili hiyo” alisema Kunambi.
Alisema hizi ni juhudi za kutekeleza kampeni ya Dodoma ya Kijani ambayo ina lengo la kulifanya Jiji la Dodoma na Mkoa mzima kustawisha miti ya kutosha ili kuhifadhi mazingira yatakayokuwa rafiki zaidi kwa maisha ya binadamu.
Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa TFS Profesa Silayo alisema kuwa tayari taasisi yake imetenga Shilingi Milioni 300 kwa ajili ya kuanza kutekeleza mpango huo alioutaja kuwa wa Kihistoria kwani haujawahi kufanyika katika Halmashauri yeyote Nchini, na kwamba utalipa hadhi kubwa Jiji la Dodoma kwenye Jumuiya ya Kimataifa.
“Makubaliano haya yataliweka Jiji la Dodoma katika ramani ya dunia katika kwenda na mahitaji ya maendeleo endelevu ya dunia kupitia mpango uendelevu wa Miji, lazima tujipange kukabiliana na ongezeko la watu na ukuaji wa Miji, Mpango huu utalifanya Jiji hili kwenda sambamba na kuweka uwiano sawia wa kiikolojia.” Alisema Profesa Silayo.
Makubaliano hayo yamesainiwa ikiwa ni takribani wiki mbili baada ya Jiji la Dodoma kuingia makubaliano na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCA) ya utunzaji wa mizunguko mitatu mikubwa ya barabara iliyopo Jijini humo, ambapo Mamlaka hiyo itahudumia bustani za maua na kuweka sanamu za Wanyama ikiwemo ya Tembo ili kupendezesha Mji na kutangaza vivutio vya kitalii vilivyopo Nchini.  


Monday, June 25, 2018

MATIBABU YA KIBINGWA HOSPITALI TEMBEZI YAANZA LEO JUNI 25 JIJINI DODOMA





.................................................................
HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imeanza rasmi zoezi la siku 5 la kutoa huduma ya matatibu kwa wagonjwa mbalimbali kwa mfumo wa Hospitali Tembezi linalofanyika katika Hospitali Teule ya Wilaya Mtakatifu Gemma iliyopo Kata ya Miyuji Jijini humo.
Mganga Mkuu wa Jiji la Dodoma Hamad Nyembea amesema huduma ya Hospitali Tembezi ni jukwaa linalowakutanisha madaktari Bingwa wa fani mbalimbali za utabibu kama mgonjwa ya akina mama na watoto, Figo, Moyo, Koo na Pua, Kinywa na Meno, Shinikizo la Damu, Sukari, Tezi Dume, Shingo ya Kizazi, Macho, Masikio, pamoja na upasuaji wa mifupa na wa kawaida.
Ametoa wito kwa wakazi wa Jiji la Dodoma na Wilaya za jirani hususan wanaosumbuliwa na maradhi mbalimbali kutumia fursa hiyo vizuri.
"Kuna wagonjwa wengine ambao wameandikiwa rufaa kwenda Hospitali za mbali kama Muhimbili Dare es Salaam na hawana uwezo, hii ni fursa kwao kwani hapa kuna madaktari Bingwa wa fani zote na watahudumia kwa muda wa siku tano kuanzia leo, mpaka Ijumaa Juni 29.
Alifafanua kuwa utaratibu wa matibabu ni wa kawaida ambapo wagonjwa wenye Bima za Afya za NHIF na CHF watatibiwa kwa kutumia kadi zao na wale wasio na Bima watachangia Shilingi elfu 5 kama gharama ya kuonana na Daktari, na kwa huduma ya upasuaji mgonjwa atachangia Shilingi elfu 30 tu.

Thursday, June 21, 2018

JIJI ‘LAMWAGA’ MAMILIONI KWA VIJANA, WANAWAKE



Kaimu Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Jiji la Dodoma Mufungo Manyama akizungumza na viongozi wa vikundi 137 vya Wanawake na Vijana wakati wa semina elekezi kwa viongozi hao kuhusu uendeshaji wa vikundi na matumizi ya fedha za mikopo kabla ya kupatiwa mkopo wa milioni 344 mapema wiki ijayo.

Kaimu Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Jiji la Dodoma Mufungo Manyama akizungumza na viongozi wa vikundi 137 vya Wanawake na Vijana wakati wa semina elekezi kwa viongozi hao kuhusu uendeshaji wa vikundi na matumizi ya fedha za mikopo kabla ya kupatiwa mkopo wa milioni 344 mapema wiki ijayo.

Kaimu Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Jiji la Dodoma Mufungo Manyama akizungumza na viongozi wa vikundi 137 vya Wanawake na Vijana wakati wa semina elekezi kwa viongozi hao kuhusu uendeshaji wa vikundi na matumizi ya fedha za mikopo kabla ya kupatiwa mkopo wa milioni 344 mapema wiki ijayo.

Kaimu Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Jiji la Dodoma Mufungo Manyama akizungumza na viongozi wa vikundi 137 vya Wanawake na Vijana wakati wa semina elekezi kwa viongozi hao kuhusu uendeshaji wa vikundi na matumizi ya fedha za mikopo kabla ya kupatiwa mkopo wa milioni 344 mapema wiki ijayo.


.....................................................
HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma inatarajia kutoa takribani shilingi milioni 500 kwa ajili ya kukopesha vikundi vya Wajasiriamali Wanawake na Vijana kwa mwaka wa fedha unaomalizika Mwezi Juni, 2018.

Jumla ya vikundi 137 vinatarajiwa kunufaika na fedha hizo zinazotokana na makusanyo ya kodi za ndani ya Halmashauri (Own Source) ambapo  vikundi vya Wanawake ni 102 na vya vijana 37.

Akizungumza wakati akitoa semina elekezi kwa viongozi wa vikundi hivyo katika ukumbi wa Shule ya Sekondari ya Dodoma leo Juni 21, 2018, Kaimu Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Jiji la Dodoma Mufungo Manyama aliwaeleza wajumbe kuwa awamu ya mwisho ya mikopo kwa mwaka huu wa fedha itatolewa katikati ya wiki ijayo ambapo jumla ya Shilingi milioni 344 zitakabidhiwa kwa vikundi hivyo.

Aliwataka Wanavikundi hao kuwa makini na matumizi ya fedha wanazokopeshwa na kufanya marejesho kwa wakati ili wapate fursa ya kukopeshwa zaidi.

Kwa upande wao, baadhi ya viongozi wa vikundi hivyo waliishukuru Halmshauri ya Jiji na kuahidi kutumia mikopo hiyo kwa malengo yaliyokusudiwa ili waweze kurejesha kwa wakati hali itakayopelekea kunufaisha vikundi vingi zaidi.



Tuesday, June 5, 2018

WAKAZI DODOMA WAASWA KUKIJANISHA JIJI


Wadau mbalimbali katika Maandamano kuelekea Viwanja vya Nyerere Square Jijini Dodoma wakati wa kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani leo Juni 5, 2018.
Afisa Mazingira kutoka Idara ya Mazingira na Udhibiti wa Takangumu Jiji la Dodoma Ally Mfinanga akitoa neno la utangulizi kwa Mgeni rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani Naibu Meya wa Jiji hilo Jumanne Ngede (hayupo pichani) na wadau wengine katika Viwanja vya Nyerere Square leo Juni 5, 2018.

Mgeni Rasmi Naibu Meya Jumanne Ngede (wa pili kulia) akikagua mabanda ya wadau wa Mazingira

Mgeni Rasmi Naibu Meya Jumanne Ngede (wa pili kushoto) akikagua mabanda ya wadau wa Mazingira





....................................................................


NAIBU Meya wa Halmshauri ya Jiji la Dodoma Jumanne Ngede ametoa wito kwa kila mkazi wa Jiji hilo kuhakikisha anatunza Mazingira kwa kupanda miti katika maeneo yanayomzunguka ili kuunga mkono juhudu za Serikali na wadau kuhakikisha Jiji linakuwa la kijani kwa manufaa ya viumbe vyote.
Alitoa wito huo mapema leo asubuhi alipotembelea na kukagua mabanda ya wadau mbalimbali wa Mazingira walioshiriki kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere vilivyopo katikati ya Jiji la Dodoma leo Juni 5, 2018.   

Mhe. Ngede aliwapongeza wadu mbalimbali hususan wanaojihusisha na nishati mbadala kama Gesi na Sola ambazo matumizi yake yanasaidia kupunguza  ukataji wa miti na uharibufu wa misitu kwa ajili ya kuchoma mkaa unaotumika kwa kazi za jikoni.

Kwa upande wake, Afisa Mazingira kutoka Idara ya Mazingira na Udhibiti wa Takangumu Jiji la Dodoma Ally Mfinanga alisema Halmashauri imekuwa ikishikiana na wadau mbalimbali ili kuhakikisha kila kundi katika jamii linawajibika katika kutunza Mazingira.

“Kuna wadau ambao tunashirikiana nao katika kutunza Mazingira kwa maana ya kupanda miti na kutunza misitu lakini pia, kama Halmashauri tunajukumu la kusafisha Mazingira kwa kuondosha taka zinazozalishwa Mjini…haya yote tunayatekeleza kwa kuwashirikisha pia wadau kama TFS na vikundi mbalimbali, vikiwemo vya kuzoa taka” alisema Mfinanga.

Kilele cha siku ya Mazingira Duniani huadhimishwa Juni 5 kila Mwaka na huambatana na jumbe mbalimbali kama sehemu ya kueleimisha Jamii, ambapo kaulimbiu ya Mwaka huu inasema “Mkaa ni gharama, tumia nishati mbadala”.


Wednesday, May 30, 2018

JIJI LA DODOMA VINARA UMISETA


Mkuu wa Idara ya Elimu Sekondari wa Jiji la Dodoma Mwalimu Abdallah Membe akionesha kikombe cha ubingwa wa Michezo ya UMISETA Kimkoa iliyofanyika kwa siku tatu katika Viwanja vya Sekondari ya Dodoma kuanzia Mei 26 mwaka huu. 
Mkuu wa Idara ya Elimu Sekondari wa Jiji la Dodoma Mwalimu Abdallah Membe akipokea kikombe cha ubingwa wa Michezo ya UMISETA Kimkoa iliyofanyika kwa siku tatu katika Viwanja vya Sekondari ya Dodoma kuanzia Mei 26 mwaka huu. 
Washiriki wakiwa wameketi kando ya vikombe vilivyotolewa kwa washindi


..................................................

HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imeibuka mshindi wa jumla baada ya kushinda michezo mingi katika michezo ya Shule za Sekondari (UMISETA) iliyofanyika kwa siku tatu kuanzi Mei 26, 2018 na kushirikisha zaidi ya Wanamichezo 700 kutoka katika Wilaya zote za Mkoa wa Dodoma, huku Wilaya ya Kongwa ikishika nafasi ya pili na Mpwapwa nafasi ya tatu.

Timu ya Wanamichezo wa Jiji la Dodoma iliibuka bingwa wa Mkoa baada ya kushinda michezo ya Mpira wa Mikoni kwa Wavulana, Mpira wa Pete, Mpira wa Miguu kwa Wasichana, Kikapu kwa Wavulana na Wasichana, kurusha tufe, kurusha kisahani,
na riadha kwa mita 200.

Mkuu wa Idara ya Elimu Sekondari wa Jiji la Dodoma Mwalimu Abdallah Membe amesema amefurahishwa na ushindi walioupata na kwamba wao kama Jiji walijipanga vizuri, huku akiwapongeza wote waliofanikisha mafanikio hayo wakiwemo Wanafunzi, Walimu, na wadau wengine wote.

Amesema baada ya hatua hiyo kufikia tamati, timu ya Mkoa ya Michezo hiyo itasafiri Jumapili wiki hii kuelekea Jijini Mwanza kushiriki michezo hiyo kwa ngazi ya Taifa inayotarajiwa kuanza Jumatatu Mei 4 mwaka huu Jijini humo.


Saturday, May 26, 2018

WAZIRI JAFFO: JIJI LA DODOMA NI MFANO NCHINI KUWATAMBUA WAZEE


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali (TAMISEMI) Selemani Jaffo akimkabidhi kitambulisho rasmi cha kumtambua mmoja ya Wazee wa Kata ya Mkonze Halmashauri ya Jiji la Dodoma wakati Waziri huyo alipozindua zoezi hilo mapema leo Mei 26, 2018. Wanaoshudia ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi (kulia kwa Waziri) na Mkurugenzi wa Jiji hilo Godwin Kunambi (mwenye shati jeupe). Kushoto kwa Waziri aliyevaa miwani ni Mganga Mkuu wa Jiji la Dodoma Hamadi Nyembea.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali (TAMISEMI) Selemani Jaffo (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na badhi ya Waze wa Kata ya Mkonze Jijini Dodoma baada ya kuzindua na kuwakabidhi vitambulisho rasmi vya kuwatambua  Wazee katika Halmashauri ya Jiji hilo mapema leo Mei 26, 2018. Kulia ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi na kushoto ni Mkurugenzi wa Jiji hilo Godwin Kunambi (mwenye shati jeupe). 
Baadhi ya Wazee wa Kata ya Mkonze Jijini Dodoma wakifuatilia hafla ya uzinduzi wa utaoji wa vitambulisho vya Wazee uliofanywa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI Selemani Jaffo leo Mei 26, 2018.
Diwani wa Kata ya Mkonze Jiji la Dodoma David Bochela akitoa neno wakati wa hafla ya uzinduzi wa utaoji wa vitambulisho vya Wazee uliofanywa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI Selemani Jaffo leo Mei 26, 2018 katika Kata hiyo.

...........................................................................


WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Selemani Jaffo amesema, Halmashauri ya Jiji la Dodoma ni ya mfano Nchini katika kuwatambua na kuwatengenezea vitambulisho maalum vya kuwatambulisha Wazee katika maeneo ya huduma mbalimbali ikwemo matibabu, akiwa ni utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Wazee ya mwaka 2003 inayolenga katika  kuhakikisha kuwa, Wazee wa Tanzania wanatambuliwa na wanapewa fursa ya kushiriki katika mambo yanayohusu maisha ya kila siku na kupata huduma zote za msingi.

Waziri Jaffo ameyasema hayo mapema leo Mei 26, 2018, alipokuwa akizindua rasmi zoezi la utoaji wa vitambulisho vya Wazee kwenye hafla fupi iliyofanyika katika Kata ya Mkonze iliyopo umbali wa kilometa 4.7 kutoka katikati ya Jiji la Dodoma.

Akizungumza wakati wa  hafla hiyo ambayo pia ilihudhuriwa na Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi na Mkurugenzi wa Jiji hilo Godwin Kunambi, Waziri huyo aliagiza Halmashauri za Mikoa yote 26 ya Tanzania Bara  kuhakikisha zinawatambua Wazee katika maeneo yao na kuwasilisha taarifa kamili ya kila Mkoa kuhusu Wazee katika  Ofisi yake ifikapo Juni 30, mwka huu.

Awali, akiwasilisha taarifa ya utekeleaji wa zoezi hilo kwa niaba ya Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Godwin Kunambi, Mganga Mkuu wa Jiji hilo Hamadi Nyembea alisema Halmashauri ilianza zoezi hilo kwa kuwatambua Wazee katika Kata zote 41 za Jiji la Dodoma, na kwamba mpaka sasa jumla ya Wazee 15, 854 wameshatambuliwa kutoka katika Kata 33, sawa na asilimia 80.5.

Alisema, hatua iliyofuata ni kuwapiga picha Wazee waliotambuliwa na kuwatengenezea vitambulisho, zoezi lililoanza rasmi mwezi Februari Mwaka huu, ambapo jumla ya Wazee 1,118 wameshapigwa picha katika Kata za Mkonze, Mnadani, Uhuru, Madukani, Makole na Majengo na kwamba kazi hiyo inaendelea katika Kata zilizobaki.

“Jumla ya vitambulisho 564 vya Wazee vimeshakamilika na wahusika watakabidhiwa rasmi leo kwa ajili ya kuanza kuvitumia” alisema Mganga Mkuu huyo wakati akiwasilisha taarifa hiyo.


Friday, May 25, 2018

MKURUGENZI JIJI LA DODOMA ATANGAZA NEEMA KWA WATEJA WA VIWANJA


Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Godwin Kunambi (kulia) akizungumza na Waandishi wa Habari leo ambapo ameongeza muda wa wateja wa Viwanja kulipa gharama za Viwanja vyao kutoka Mwezi mmoja wa awali hadi miezi mitatu sasa.
Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Godwin Kunambi (kulia) akizungumza na Waandishi wa Habari leo ambapo ameongeza muda wa wateja wa Viwanja kulipa gharama za Viwanja vyao kutoka Mwezi mmoja wa awali hadi miezi mitatu sasa.

Mtaalamu wa Jiji la Dodoma akimuelekeza mteja kwenye ramani inayoonesha mgawanyo wa Viwanja ili aweze kuchagua kiwanja kwa mujibu wa mahitaji yake katika zoezi la uuzwaji wa Viwanja linaloendelea sasahivi katika Halmashauri ya Jiji hilo.
Ramani ya Tanzania ikionesha Jiji la Dodoma lilipo kutoka katika Mikoa mingine yote ya Tanzania.

..............................................................................


HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imeongeza muda wa kulipia Viwanja kwa wateja wake wote walionunua Viwanja kuanzia Aprili 20, mwaka huu kutoka siku 30 yaani Mwezi mmoja hadi siku 90 yaani miezi mitatu.

Aidha, Halmashauri hiyo inatarajia kuendelea kuuza Viwanja vya eneo la Iyumbu kuanzia tarehe 5 Juni, 2018 kwani tayari imeshamaliza kazi ya kushughulikia malalamiko ya Wakazi wa Ngaloni walioibuka na kudai kutolipwa fidia hapo awali.

Hayo yametangazwa na Mkurugenzi wa Jiji hilo Godwin Kunambi wakati akiongea na Waandishi wa Habari Jijini humo leo ambapo amesema Halmashauri imefikia uamuzi huo baada ya kuridhika na mwenendo wa wateja kulipia Viwanja vyao ambapo mpaka sasa zaidi ya shilingi bilioni 4 zimeshalipwa kwa Wananchi kama fidia ya maeneo yao yaliyotwaliwa wakati wa upimaji.

Alitoa wito kwa wateja wote walionunua viwanja na wanaoendelea kununua kutumia muda ulioongezwa kama fursa ya kukamilisha malipo yao ili kuepuka usumbufu usio wa lazima baada ya muda huo kumalizika.

“Kwa wale wote waliokuwa wanasubiri Viwanja vya Iyumbu wafike katika eneo letu la kuuzia Viwanja ambalo ni Ofisi za Manispaa ya zamani jirani na Sabasaba siku ya tarehe 5 mwezi ujao…tutaanza kuviuza siku hiyo” alisema Kunambi.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi huyo wa Jiji ametoa muda wa miezi mitatu kwa watu wote waliopewa Viwanja na iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) katika maeneo ya Njedengwa, Miganga, Mkonze, Iyumbu New Town Center, na Mkalama na hawajakamilisha malipo ya Viwanja hivyo kukamilisha ndani ya kipindi hicho vinginevyo Halmashauri itavitwaa kwa mujibu wa Sheria na kuviuza kwa wateja wengine wenye mahitaji.  


Thursday, May 24, 2018

‘VITA’ SARATANI YA SHINGO YA KIZAZI YAZINDULIWA DODOMA


Mwanafunzi wa Kidato cha pili katika shule ya Sekondari ya Dodoma Huda Khalid Rabash akionesha kadi yake aliyokabidhiwa na Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi (kushoto) kama ishara ya uzinduzi rasmi wa utoaji wa chanjo ya kinga dhidi ya ugonjwa wa Saratani ya Shingo ya kizazi kwa Wanawake. Kadi hiyo itamuwezesha kupata chanjo hiyo kwa awamu ya pili baada ya miezi sita ili kukamilisha kinga yake dhidi ya ugonjwa huo. Wengine wanaoshuhudia ni Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Hamadi Nyembea (mwenye miwani katikati nyuma)  na Mkuu wa Shule hiyo Mwalimu Amani Mfaume (mwenye miwani katikati mbele). Kushoto ni Mwalimu wa Afya wa Shule hiyo Caritas Burchard. PICHA ZOTE: RAMADHANI JUMA-OFISI YA MKURUGENZI
Muhudumu wa Afya Ruth Azaliwa akimchoma Sindano ya chanjo dhidi ya Saratani ya Shingo ya Kizazi kwa Wanawake Mwanafunzi wa kidato cha pili wa Shule ya Sekondari ya Dodoma Huda Khalid Rabash kuashiria uzinduzi wa zoezi la utoaji wa chanjo hiyo katika Wilaya ya Dodoma jana. Wanaoshuhudia ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi (kushoto) na Mwalimu wa Afya wa Shule hiyo Caritas Burchard (kulia).
Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi akimkabidhi kadi maalum kwa ajili kupata huduma ya chanjo awamu ya pili dhidi ya ugonjwa wa Saratani ya Shingo ya kizazi kwa Wanawake Mwanafunzi wa kidato cha pili wa Shule ya Sekondari ya Dodoma Huda Khalid Rabash kama ishara ya uzinduzi wa zoezi la utoaji wa chanjo hiyo katika Wilaya ya Dodoma jana katika ukumbi wa Shule hiyo.  
Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Hamadi Nyembea akizungumza wakati wa uzinduzi wa zoezi la utoaji wa chanjo dhidi ya ugonjwa wa Saratani ya Shingo ya kizazi kwa Wasichana walio chini ya umri wa miaka 14 katika Wilaya ya Dodoma jana. Katikati ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi na wa kwanza ni Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Dodoma palikofanyika uzinduzi huo Mwalimu Amani Mfaume. 
Sehemu ya Wanafunzi wa kike wa Shule ya Sekondari ya Dodoma wakifuatilia shughuli ya uzinduzi wa utoaji wa chanjo dhidi ya ugonjwa wa Saratani ya Shingo ya Kizazi  uliofanyika katika Shule hiyo jana.
Zoezi la utoaji wa chanjo dhidi ya ugonjwa wa Saratani ya Shingo ya kizazi kwa Wasichana walio chini ya umri wa miaka 14 likiendelea katika Sekondari ya Dodoma mara baada ya kuzinduliwa rasmi na Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi.


................................................

ZOEZI la utoaji wa chanjo ya kinga dhidi ya ugonjwa wa Saratani ya Shingo ya Kizazi kwa Wanawake limezinduliwa rasmi katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma huku wasichana waliopatiwa chanjo hiyo wakitoa wito kwa wenzao kujitokeza na kuhakikisha wanakingwa dhidi ya ugonjwa huo.

Uzinduzi huo umefanyika jana katika ukumbi wa Dodoma Sekondari ambapo mgeni rasmi katika hafla fupi ya uzinduzi huo alikuwa Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Deo Ndejembi huku Mganga Mkuu wa Halmashauri Hamadi Nyembea akimwakilisha Mkurugenzi Godwin Kunambi.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Kaimu Mkuu huyo wa Wilaya alisema uzinduzi huo ni kiashiria cha kuwafikia Wasichana wote wenye chini ya umri wa miaka 14 ndani ya Wilaya ya Dodoma.
Alisema zoezi hilo litaendeshwa na Halmashauri kupitia Ofisi ya Mganga Mkuu, na litashirikisha viongozi wa ngazi zote ikiwemo Kata na Mitaa ili kuhakikisha kila msichana anayehusika anafikiwa na kupatiwa chanjo hiyo.

Awali, Mganga Mkuu wa Halmashauri Hamadi Nyembea alisema katika kipindi cha Mwaka mmoja ujao, jumla ya Wasichana 7,828 walio na umri wa chini ya miaka 14 wanatarajiwa kufikiwa na kupatiwa chanjo hiyo katika Wilaya ya Dodoma.

Alisema  baada ya miezi sita Wasichana wote waliopatiwa chanjo hiyo watapatiwa tena kwa awamu ya pili ili kukamilisha kinga yao dhidi ya virusi vinavyoeneza ugonjwa huo.

Alimweleza Mgeni rasmi na wajumbe kuwa, chanjo hiyo imethibitishwa na Shirika la AfyaDuniani (WHO) hivyo Wasichana na Wazazi wasiwe na mashaka badala yake watoe ushirikiano wa kutosha ili kufikia lengo la Serikali la kutokomeza ugonjwa huo kama ilivyofanya kwa magonjwa kama Polio.

Tuesday, May 22, 2018

NAIBU WAZIRI LUGOLA APONGEZA UJENZI DAMPO LA KISASA


Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola (mwenye sare ya bluu) akipata maelezo jinsi mzani uliopo katika Dampo la kisasa la kuhifadhia taka lililopo Chidaya Manispaa ya Dodoma unavyofanya kazi kwa njia ya Kompyuta, kutoka kwa Mhandisi wa Mazingira wa Halmashauri hiyo Barnabs Faida.  
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola (mwenye sare ya bluu) akifuatilia maelekezo ya jinsi maabara ya kupima kemikali kwenye maji ya ardhini katika eneo la Dampo la kisasa la Halmashauri ya  Manispaa ya Dodoma inavyofanya kazi ili kuhakikisha nuwepo wa Dampo hilo hauhatarishi vyanzo vya maji katika maeneo ya jirani. Anayetoa maelezo ni Afisa Mazingira kutoka Idara ya Mazingira na Udhibiti wa Taka Ngumu ya Halmashauri hiyo  Happynes Pastory.
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola (wa tatu kushoto) akiwa katika eneo la Dampo la kisasa la kuhifadhia taka lililopo Chidaya Manispaa ya Dodoma alipofanya ziara kukagua Mifumo ya usimamizi wa Mazingira katika Dampo hilo inavyofanya kazi. Wa pili kushoto ni Diwani wa Kata ya Ntyuka Theobald Maina.
Sehemu ya Dampo iliyoanza kutumika
Sehemu ya pili ya Dampo ambayo itatumika baada ya sehemu ya kwanza kujaa

...................................................................

NAIBU Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Kangi Lugola ameipongeza Halmashauri ya Manispaa Dodoma kwa ujenzi wa Dampo la kisasa la kuhifadhia taka kwa teknolojia ya kuzizika ardhini (Sanitary Land Fill) lililopo eneo la Chidaya Kata ya Matumbulu katika Halmashauri hiyo.

Alitoa pongezi hizo jana baada ya kufanya ziara katika Dampo hilo kwa lengo la kukagua mifumo ya usimamizi wa Mazingira.
“Mfikishieni Mkurugenzi wa Halmashauri salamu zangu…nimeridhika na uendeshaji wa Dampo hili na jinsi mnavyozingatia na kusimamia usalama wa Mazingira” alisema Naibu Waziri huyo.

Alisema ni fahari kubwa kwa Halamshauri ya Manispaa ya Dodoma kuwa na Miundombinu ya kisasa ya usafi na kutaka taka zote zinazozalishwa ziondolewe na kupelekwa katika Dampo hilo ili kufiki malengo ya mradi huo.

Dampo hilo lilianza kujengwa mwaka 2010 na hadi linakamilika limegharimu zaidi ya Shilingi bilioni 7.1 ambazo ni mkopo kutoka Benki ya Dunia kupitia Serikali Kuu ikiwa ni utekelezaji wa mradi wa kuendeleza Miji ya Kimkakati Tanzania (TSCP) inayoratibiwa na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).

Naibu Waziri Lugola alikuwa katika siku ya pili ya ziara yake ya siku saba katika Wilaya ya Dodoma ambapo pamoja na mambo mengine, anakagua jinsi mifumo ya usimamizi wa Mazingira katika taasisi mbalimbali ikiwemo Hospitali na Vyuo inavyosimamiwa na kufanya kazi.


Friday, May 18, 2018

WAZIRI LUGOLA AANZA ZIARA YA WIKI MANISPAA YA DODOMA


Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola (wa pili kulia) akikagua mifumo ya usimamizi wa Mazingira katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma jana. Kushoto ni Afisa Mazingira wa Manispaa ya Dodoma Dickson Kimaro na pili kushoto ni Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mzee Nassoro. Wa tatu kutoka kulia ni Afisa Afya wa Mkoa wa Dodoma Carle Lyimo. PICHA ZOTE-RAMADHANI JUMA
Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mzee Nassoro akitoa maelezo kwa Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola (katikati) wakati wa ziara ya kiongozi huyo katika hosptali hiyo jana.
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola (kulia) akikagua mifumo ya usimamizi wa Mazingira katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma jana. Kulia ni Afisa Afya wa Mkoa wa Dodoma Carle Lyimo.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola akiwa katika sehemu ya Vyoo ya moja ya Wodi ya wagonjwa  akikagua mifumo ya usimamizi wa Mazingira katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma jana.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Kangi Lugola (kulia) akihakiki moja ya 'chemba' za mifumo ya maji katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu John wakati alipofanya ziara ya kukagua mifumo ya usimamizi wa Mazingira chuoni hapo jana.



..........................................................................


NAIBU Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Kangi Lugola ameanza ziara ya kikazi ya wiki moja katika Manispaa ya Dodoma jana ambapo alitembelea Ofisi za Halmashauri na kupokea taarifa ya hali ya Mazingira kwa ujumla iliyowasilishwa na Mkuu wa Idara ya Mazingira na udhibiti wa taka ngumu Dickson Kimaro.

Naibu Waziri pia alipata taarifa kutoka kwa wataalam wa taasisi zingine ambazo ni wadau wa Mazingira ikiwemo Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA), Idara ya Madini, na Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) ambao amefutana nao katika ziara hiyo.

Katika siku ya kwanza ya ziara yake hapo jana, Naibu Waziri Lugola alitembelea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma na Chuo Kikuu cha Mtakatifu John ambapo alikagua mifumo ya usimamizi wa taka ambapo kwa ujumla alikiri kuridhishwa jinsi taasisi hizo zinavyozingatia matakwa ya Sheria na taratibu za kuhifadhi Mazingira, lakini aliziagiza kuhakikisha takataka zinazoteketezwa kwa kuchomwa moto zinateketea kwa kiwango kinachokubalika.


Ziara ya Naibu Waziri inaendelea leo Ijumaa Mei 18, 2018 ambapo pamoja na maeneo mengine, atatembelea na kukagua mifumo ya usimamizi wa taka katika machinjio ya Punda iliyopo eneo la Kizota   na inatarajiwa kumalizika Mei 25, mwaka huu.     



Thursday, May 17, 2018

LAAC YA UGANDA ZIARANI DODOMA, YAFURAHIA MJI WA SERIAKLI


Mwakilishi wa Mkuu wa Idara ya Ujenzi wa Manispaa ya Dodoma Mhandisi Emanuel Manyanga akiwasilisha taarifa ya Miradi iliyotekelezwa na itakayotekelezwa kupitia Mradi wa Uendelezaji Miji ya Kimkakati Tanzanzia (TSCP) mbele ya Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Serikali za Mitaa ya Nchini Uganda ilipokuwa katika ziara ya kujifunza katika Manispaa hiyo jana. PICHA: OFISI YA MKURUGENZI
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Serikali za Mitaa ya Nchini Uganda Reagan Okumu (kushoto) akizungumza wakati alipowaongoza wajumbe wa Kamati hiyo katika ziara ya kujifunza katika Manispaa ya Dodoma jana.
Mhandisi wa Mazingira wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Barnabas Faida akitoa neno la utangulizi kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kwa Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Hesbu za Srikali za Mitaa ya Uganda ilipotembelea Halmashauri hiyo jana.
WAJUMBE wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa ya Bunge la Uganda wakifuatilia taarifa za miradi ya Ujenzi iliyokuwa akiwasilishwa na Mhandisi Emanuel Manyanga kutoka Idara ya Ujenzi ya Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma walipofanya ziara ya kujifunza juu ya utekelezaji wa miradi ya Kimkakati. 

............................................................

WAJUMBE wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa ya Bunge la Uganda wameishukuru Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma kwa kuipatia Serikali ya Nchi hiyo kiwanja chenye ukubwa wa eka tano katika Kata ya Mtumba eneo utakapojengwa Mji wa Serikali.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo Reagan Okumu alitoa Shukrani hizo jana wakati Kamati hiyo ilipotembelea Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma walipokuwa katika ziara ya siku moja ya kujifunza mambo mbalimbali ikiwemo utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati kama Dampo la kisasa la kuhifadhia taka kwa kuzifukia ardhini (Sanitary Land Fill) lililopo Kata ya Matumbulu ambalo ni moja ya miradi mikubwa katika eneo la usafi na utunzaji wa mazingira.

Awali akizungumza mbele ya Kamati hiyo, Mhandisi wa Mazingira wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma ambaye alimwakilisha Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Godwin Kunambi, aliwajulisha wajumbe hao kuwa, Halmashauri imetenga na kupima eneo litakalojengwa Mji wa Serikali hapa Dodoma na kwamba Serikali ya Uganda imepewa kiwanja chenye ukubwa wa eka tano kwa ajili ya matumizi ya kiofisi, ambapo pia walioneshwa ramani ya eneo hilo.

Wajumbe wa Kamati hiyo waliezea kufurahishwa kwao na hatua hiyo huku wakiahidi kufikisha taarifa hizo njema kwa Wananchi wa Uganda mara watakaporejea Nchini humo.