Friday, December 8, 2017

WALIOVUNJIWA VIBANDA KWENYE HIFADHI YA RELI DODOMA WAPATIWA ENEO NA MANISPAA


Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (wa pili kushoto) akiteta jambo na wafanyabiashara wakati akitoka katika eneo la Stendi ya Jamatini Mjini Dodoma baada ya kuzungumza na wafanyabiashara waliovunjiwa vibanda vyao kupisha mradi wa ujenzi wa Reli ya Kisasa.


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi Vijana na Ajira ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Dodoma Anthony Mavunde (wa pili kushoto) akizungumza katika mkutano na Wafanyabiashara wa eneo la Jamatini Manispaa ya Dodoma baada ya Vibanda vyao kubomolewa Kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli (RAHCO) kupisha mradi wa ujenzi wa Reli kisasa. Kulia ni Naibu Meya wa Manispaa ya Dodoma Jumanne Ngede na wa pili kulia ni Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Godwin Kunambi. Kushoto ni Katibu wa Wafanyabiashara hao John Banda.
Baadhi ya wafanyabiashara wa eneo la Jamatini Manispaa ya Dodoma wakifuatilia mkutano wao na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi Vijana na Ajira ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Dodoma Anthony Mavunde, Naibu Meya wa Manispaa ya Dodoma Jumanne Ngede na Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Godwin Kunambi.


                  ..............................................

HALMASHAURI ya Manispaa ya Dodoma inatarajia kuwapatia eneo wafanyabiashara zaidi ya 550 waliovunjiwa vibanda vyao na kampuni hodhi ya Rasilimali za Reli (RAHCO) katika stendi ya mabasi madogo ya  Jamatini ili kupisha utekelezaji wa mradi wa Reli ya kisasa, ili waendelee kufanya biashara zao kama kawaida.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi amewaeleza wafanyabiashara hao kuwa, Manispaa iko katika hatua za mwisho kuandaa eneo la Makole D-Center kwa kuweka miundombinu muhimu ikiwemo mfumo wa maji safi na maji taka ili wafanyabiashara hao waanze kufanya shughuli zao mara moja na katika mazingira rafiki na salama katika eneo hilo.

Aliyasema hayo alipotembelea eneo la Jamatini na Stendi Kuu Novemba 6 mwaka huu, akiambatana na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi Vijana na Ajira Anthony Mavunde ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Dodoma, pamoja na Naibu Meya wa Halmashauri ya Manispaa hiyo Jumanne Ngede kwa lengo la kuwapa pole wafanyabiashara hao na kuwajulisha hatua zilizochukuliwa na Viongozi mbalimbali katika kuhakikisha tatizo linalowakabili linapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

 Aliwatoa hofu ya kuwa eneo hilo halitakuwa na wateja wengi kama ilivyokuwa eneo la stendi ya Jamatini, ambapo aliwaambia tayari Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Daktari Binilith Mahenge ametoa maelekezo kwa Manispaa na Sumatra kuhakikisha daladala zinakuwa na ruti inayopita katika eneo hilo jipya la biashara ambapo abiria watakuwa na kituo cha kupanda na kushuka na hivyo kuongeza mzunguko wa wateja katika eneo hilo, na kwamba utekelezaji wa maelekezo hayo umeshaanza kufanyiwa kazi na Sumatra.

Akizungumza na wafanyabiashara ya usafiri wa mabasi katika Stendi Kuu ya mabasi ya mikoani, Mkurugenzi Kunambi aliwaambia kuwa, Manispaa kwa kushauriana na uongozi wa Mkoa na wadau kama Sumatra imepanga kuhamishia Stendi hiyo katika eneo la Chaduru au kwenye eneo la viwanja vya Nanenane vilivyopo Kata ya Nzuguni barabara kuu ya Dodoma-Dar es Salaam.

Alisema Manispaa itazungumza na uongozi wa wasafirishaji ili kupata mapendekezo yao  juu ya eneo rafiki zaidi miongoni mwa maeneo hayo mawili.


Kwa upande wake, Naibu Waziri Mavunde aliwataka wote walioathiriwa na zoezi hilo la bomoabomoa wawe watulivu katika kipindi hiki kigumu wakati Mamlaka na Viongozi wakifanya juhudi za makusudi kuwatafutia maeneo rafiki kwa shughuli zao huku Naibu Meya Ngede akiwahakikishia kuwa Baraza la Madiwani litasimamia kikamilifu suala la upatikaaji wa maeneo hayo.

Thursday, December 7, 2017

MKURUGENZI MANISPAA YA DODOMA AMALIZA HOFU YA WAFANYABIASHARA 2,500

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi akizungumza na wafanyabiashara wa soko la Sabasaba (hawapo pichani) Mjini Dodoma jana ambapo aliwahakikishia kuwa hawatahamishwa katika soko hilo. 

Sehemu ya Wafanyabiashara ya Manispaa ya Dodoma wakimsikiliza Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (hayupo pichani) wakati wa mkutano wa Mkurugenzi huyo na wafayabiashara wa soko hilo jana.
Naibu Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya DodomaJumanne Ngede akizungumza na wafanyabiashara wa soko la Sabasaba Mjini Dodoma jana ambapo alifuatana na Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi. 

Monday, December 4, 2017

USAFI WA MAZINGIRA DODOMA SASA KILA WIKI, WATAKAOKAIDI FAINI 50,000 AU JELA MIEZI 6


Mkuu wa Idara ya Mazingira na Usafishaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Dickson Kimaro  (kushoto) akifuatilia usafishaji wa barabara na mitaro katika barabara ya Dodoma-Singida wakati wa zoezi la usafi wa Mazingira unaofanywa kila Jumamosi ikiwa ni Kampeni iliyoanzishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Daktari Binilith Mahenge.
Mheshimiwa Diwani wa Kata ya Uhuru Manispaa ya Dodoma Ally Kheri (kulia) akishiriki zoezi la usafi wa Mazingira katika Mtaa wa Barabara ya 8 katikati ya Mji wa Dodoma wakati wa zoezi la usafi wa Mazingira unaofanywa kila Jumamosi ikiwa ni Kampeni iliyoanzishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Daktari Binilith Mahenge.
........................................

HALMASHAURI ya Manispaa ya Dodoma imepanga kutumia askari wa Mgambo 30 watakaokuwa wanafanya doria katika viunga vya Mji ili kudhibiti watu wanaochafua mazingira kwa kutupa taka ovyo ikiwa ni namna mojawapo ya kuhakikisha mji huo unakuwa safi wakati wote ikizingatiwa kuwa ndiyo Makao Makuu ya Nchi.

Hatua hiyo inafuatia kampeni ya usafi wa mazingira iliyoanzishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Daktari Binilith Mahenge ya kufanya usafi siku ya Jumamosi kila wiki.

Akizungumza wakati wa zoezi la usafi mwishoni mwa Wiki iliyopita, Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi amesema askari Mgambo 30 waliofuzu mafunzo wako tayari na kwamba Manispaa inatarajia kuanza kuwatumia wiki hii ya kwanza ya mwezi Desemba.  


Aliwashauri wakazi wa Dodoma na wageni kujiepusha na utupaji wa taka ovyo, na kwamba atakayebainika na kuthibitika kufanya hivyo atatozwa faini kati ya Shilingi 50,000 hadi 300,000 kulingana na mazingira ya tukio papo hapo na endapo atashindwa kulipa atatumikia kifungo cha miezi sita gerezani.

Tuesday, November 28, 2017

UPIGAJI CHAPA MIFUGO WAENDELEA KUSHIKA KASI MANISPAA YA DODOMA


Ofisa mifugo wa Kata ya Chahanga katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma William Gervas akimpiga chapa Ng'ombe wakati wa zoezi la upigaji chapa mifugo linaloendelea katika Halmashauri hiyo.




                                                 

Monday, November 27, 2017

RC MAHENGE ATAKA MAMBO MATANO KUIPAISHA DODOMA

Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Chamwino Vumilia Nyamoga (wa pili kushoto) akizungumza wakati wa ziara ya kujitambulisha ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dokta Binilith Mahenge (wa tatu kulia) Wilayani humo. Wa kwanza kulia ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma Rehema Madenge na wa pili ni Meya wa Manispaa ya Dodoma Mstahiki Profesa Davis Mwamfupe. Kushoto ni Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma Rehema Madenge  akizungumza wakati wa ziara ya kujitambulisha ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dokta Binilith Mahenge katika Wilaya ya Dodoma ambapo alizungumza na watumishi wa Manispaa katika ukumbi wa Manispaa Novemba 24 mwaka huu.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (kushoto) akiwasilisha taarifa ya maendeleo ya Wilaya ya Dodoma kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dokta Binilith Mahenge (aliyevaa miwani katikati) wakati wa ziara ya kujitambulisha ya Mkuu huyo wa Mkoa katika Wilaya ya Dodoma. Wa kwanza kulia ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma Rehema Madenge na wa pili ni Meya wa Manispaa ya Dodoma Mstahiki Profesa Davis Mwamfupe. 

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dokta Binilith Mahenge akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma wakati alipokuwa katika ziara ya kujitambulisha katika Wilaya ya Dodoma Novemba 24 mwaka huu. Wa kwanza kulia ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma Rehema Madenge na wa pili ni Meya wa Manispaa ya Dodoma Mstahiki Profesa Davis Mwamfupe. PICHA ZOTE NA RAMADHANI JUMA-OFISI YA MKURUGENZI WA MANISPAA

.......................................

MKUU wa Mkoa wa Dodoma Dokta Binilith Mahenge amewataka watumishi na viongozi wa Halmashauri Mkoani humo kuhakikisha wanayapa kipaumbele  mambo matano ikiwemo kudumisha hali ya Ulinzi na Usalama ambayo  ndiyo nguzo muhimu  inayopelekea shughuli nyingine za maendeleo kufanyika kwa ufanisi ili kuifanya Dodoma ikue kwa kasi.

Mambo mengine aliyoyayaorodhesha Mkuu huyo wa Mkoa kama dira ya kuharakisha maendeleo ni pamoja na utayari wa kubadilika kwa watumishi na kutofanya kazi kwa mazoea, utoaji wa huduma bora na zenye viwango kwa wananchi, kudumisha dhana ya Ushirikishwaji baina ya Taasisi na miongoni mwa watumishi, na kuepuka migogoro baina ya watumishi ndani ya Taasisi hali inayoweza kudumaza malengo ya Serikali katika kuwadumia wananchi.

Mkuu wa Mkoa Mahenge aliyasema hayo wakati alipokuwa akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma alipofanya ziara ya kujitambulisha katika Wilaya ya Dodoma Novemba 24 mwaka huu.


Awali alipokea taarifa ya maendeleo ya Wilaya iliyowasilishwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi kwa niaba ya Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Chamwino Vumilia Nyamoga.

MACHINGA MANISPAA YA DODOMA KUKABIDHIWA ENEO RASMI HIVI KARIBUNI, BIBI KIZEE AISHUKURU MANISPAA

Bibi aliyejengewa nyumba na Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma baada ya kuondolewa kwenye eneo la Makole D-Center lililotengwa na Manispaa kwa ajili ya Wafanyabiashara wadogo 'Machinga'  Elizabeth Sonyo mwenye umri wa miaka zaidi ya 75 akiwa nje ya makazi yake mapya katika Kata ya Makole Mjini Dodoma.



..........................................

WAFANYABIASHARA wadogo maarufu kama Machinga katika Manispaa ya Dodoma wanatarajiwa kupewa eneo lililotengwa  rasmi na Halmashauri ya Manispaa hiyo kwa ajili ya biashara zao lililopo katika Kata ya Makole mjini humo.

Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma chini ya Mkurugenzi Godwin Kunambi imekamilisha uwekaji wa miundombinu muhimu katika eneo hilo maarufu kama ‘Makole D-Center’ ikiwemo choo, ambapo wakati wowote wafanyabiashara hao watahamishiwa kwa utaratibu utakaoratibiwa na Manispaa kwa kushirikiana na uongozi wa wafanyabiashara hao.

Katika hatua za awali za maandalizi ya  eneo hilo, Halmashauri pamoja na mambo mengine, iliondoa makazi ya Bibi Elizabeth Sonyo aliyekuwa akiishi katika eneo hilo kinyume cha Sheria.

Hata hivyo, kutokana na Bibi huyo anayekadiriwa kuwa na umri wa zaidi ya miaka 75 kutokuwa na uwezo wa kujenga, Manispaa ilibeba jukumu la kumjengea makazi mapya na bora zaidi katika eneo jingine, ambapo amemshukuru Mkurugenzi wa Manispaa kwa kitendo hicho kwani hakuwa na uhalali wa kisheria wa kuishi katika hilo na kwamba angeweza kuondolewa bila kupewa msaada wowote.  

Kwa mujibu wa Kaimu Mhandisi wa Ujenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Ludigija Ndwata, kazi iliyobaki ni kuweka mawe maalum (gravels) katika eneo hilo ili livutie zaidi na liwe rafiki kwa wafanyabiashara na wateja, kabla ya matumizi kuanza.


Halmashauri ya Manispaa pia inaandaa eneo la ‘Chaduru D-center’ kwa ajili ya kulirasimisha kwa matumizi ya wafanyabiashara wadogo hususan akina mama wanaouza vyakula, mbogamboga, na matunda. 

Thursday, November 16, 2017

WAKAZI 8570 MKONZE MANISPAA YA DODOMA WAPATIWA HUDUMA YA MAJI SAFI YA BOMBA


Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) Mh. Vedasto Ngombale (wa tatu kushoto) akizungumza wakati Kamati hiyo ilipotembelea mradi wa Maji katika Kata ya Mkonze Manispaa ya Dodoma jana.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (wa pili kulia) akitoa ufafanuzi wakati alipowasilisha taarifa ya mradi wa Mkonze mbele ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) ilipotembelea na kukagua mradi huo jana.

...............................................

WANANCHI 8570 wakazi wa Kata ya Mkonze katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma wananufaika na huduma ya maji safi ya bomba kufuatia kukamilika kwa mradi wa Maji katika Kata hiyo ulitekelezwa na Manispaa hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi iliyowasilishwa kweye Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), mradi huo uliotekelezwa chini ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji awamu ya kwanza, ulianza kujengwa Septemba, 2012 na kukamilika Machi, 2014 kwa gharama ya Shilingi 497,263,970 ukiwa na vituo 15 vya kutolea maji.

Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) ilitembelea mradi huo jana na kuishauri Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma kuharakisha taratibu za kukabidhi mradi huo kwa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dodoma (DUWASA) ambayo kwa mujibu wa sheria ndiyo yenye dhamana ya kutoa huduma ya Maji mjini.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mheshimiwa Vedasto Ngombale aliwaogoza wajumbe  wa Kamati yake katika ziara ya kukagua ufanisi wa mradi huo.

Akizungumza kwa niaba ya Kamati katika eneo la mradi, Mheshimiwa Ngombale ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Kilwa Kaskazini, alisema ni muhimu mradi huo kuwa chini ya DUWASA kwani umeshakamilika na uko eneo la mjini, badala ya kuwa chini ya Manispaa na kusimamiwa na Jumuiya ya Watumiaji Maji.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi aliahidi kutekeleza ushauri na maelekezo yote ya Kamati hiyo kwa wakati ili malengo ya Serikali ya kusogeza huduma muhimu karibu na wananchi yakamilike.


Tayari Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma iko katika hatua za mwisho za kukakabidhi mradi mwingine wa maji kwa DUWASA uliotekelezwa katika Kata ya Ng’hong’ona ukiwa katika hatua ya mwisho ya ukamilishwaji ambapo wananchi 8318 watanufaika na mradi huo wenye vituo 20 vya kutolea maji.