Thursday, March 8, 2018

MPANGO MKAKATI UCHUMI WA WANAWAKE DODOMA WAZINDULIWA



Mgeni Rasmi ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma Fatma Tawfiq akionesha Mpango Mkakati wa kuwawezesha Wanawake Kiuchumi Manispaa ya Dodoma mara baada ya kuuzindua jana wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Dunia iliyofanyika kwa ngazi ya Mkoa katika Kata ya Msalato Manispaa ya Dodoma. PICHA-OFISI YA MKURUGENZI WA MANISPAA.
Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma Fatma Tawfiq akikata utepe Mpango Mkakati wa kuwawezesha Wanawake Kiuchumi Manispaa ya Dodoma mara baada ya kuuzindua jana wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Dunia iliyofanyika kwa ngazi ya Mkoa katika Kata ya Msalato Manispaa ya Dodoma. PICHA-OFISI YA MKURUGENZI WA MANISPAA.
Mratibu wa Dawati la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi Manispaa ya Dodoma Hidaya Mizega (kulia) aliyemwakilisha Mkurugenzi wa Manispaa hiyo Godwin Kunambi katika maadhimisho ya kilele cha siku wa Wanawake Duniani iliyofanyika Kimkoa katika Kata ya Msalato Mjini Dodoma akizungumza wakati wa sherehe hizo. 
Diwani wa Kata ya Msalato Ally Mohamed akitoa neno wakati wa sherehe hizo
Kaimu wa Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii Manispaa ya Dodoma Rukia Nyange akitoa neno.
Kikosi Maalum kikiongoza maandamano ya akina mama kutoka taasisi na wadau mbalimbali wakati wa sherehe za Maadhimisho ya kilele  cha Siku ya Wanawake duniani yaliyofanyika katika Kata ya Msalato Mnaispaa ya Dodoma jana kwa ngazi ya Mkoa
Mgeni Rasmi ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma Fatma Tawfiq (wa pili kuhoto) akikagua maband ya Wajasiriamali Wanawake jana wakati wa Maadhimisho ya kilele cha Siku ya Wanawake Dunia iliyofanyika kwa ngazi ya Mkoa katika Kata ya Msalato Manispaa ya Dodoma. PICHA-OFISI YA MKURUGENZI WA MANISPAA.

..................................................

HALMASHAURI ya Manispaa ya Dodoma imezindua Mpango Mkakati wa kuwawezesha kiuchumi Wanawake na akina Mama wa Manispaa hiyo ili wajikwamue katika changamoto mbalimbali za maisha yao ya kila siku.

Mpango Mkakati huo unaotarajiwa kutekelezwa katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2018, ulizinduliwa jana Machi 8, 2018 ambapo sherehe za uzinduzi zilienda sambamba na maadhimisho ya kilele cha siku ya Wanawake Duniani zilizofanyika katika Kata ya Msalato Mjini Dodoma.

Akizindua Mpango Mkakati huo, Mbunge wa Viti Maalum wa Mkoa wa Dodoma Fatma Tawfiq alitoa wito kwa Wanawake kuungana na kuwa kitu kimoja ili kuwa kimoja ili kupambana na changamoto zinazowakabili ikiwemo za kiuchumi.
Aliwataka pia kuwa tayari kugombea na nafasi mbalimbali za uongozi ili wawe katika nafasi za maamuzi, na kwamba waanze na uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika Mwakani kabla ya ule Mkuu wa mwaka 2020.

Kwa upande wake, Mratibu wa Dawati la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi wa Manispaa ya Dodoma Hidaya Mizega ambaye alimwakilisha Mkurugenzi wa Manispaa hiyo Godwin Kunambi katika sherehe hizo alisemakuwa, Mpango Mkakati huo ndio dira ya kuwainua wanawake wa Manispaa ya Dodoma kiuchumi na kwamba yataandaliwa majukwaa mbalimbali ya Wanawake ili kuutambulisha kwa wadau.

“Wanawake wataongozwa jinsi ya kuunda vikundi vingi vya kuichumi ili kupata fursa mbalimbali wakiwa pamoja…kwa sasa Dawati la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi limeanzishwa katika kila Kata ya Manispaa ya Dodoma” alisema Mizega.

Alisema kuwa miongoni mwa malengo mahsusi ni kuwa na SACCOS ya akina mama wote wa Wilaya ya Dodoma, hivyo baada ya kipindi cha miaka mitatu ya utekelezaji wa Mpango Mkakati huo kumalizika, itafanywa tathmini ya kina kuhusu mafanikio na changamoto zilizojitokeza ili zifanyiwe kazi.

Tuesday, February 13, 2018

WANANCHI WAUNGA MKONO BOMOA BOMOA, WANAOHAMIA DODOMA WATAHADHARISHWA


Zoezi la ubomoaji lililoendeshwa na Manispaa ya Dodoma likiwa limeanza mapema jana asubuhi katika baa maarufu Mjini Dodoma ya Chako ni Chako baada ya Mmiliki wake kudaiwa kukiuka masharti ya kibali chake cha ujenzi.
Zoezi la ubomoaji lililoendeshwa na Manispaa ya Dodoma likiwa linaendelea mapema jana asubuhi katika baa maarufu Mjini Dodoma ya Chako ni Chako baada ya Mmiliki wake kudaiwa kukiuka masharti ya kibali chake cha ujenzi.
Zoezi la ubomoaji lililoendeshwa na Manispaa ya Dodoma likiwa linaendelea mapema jana asubuhi katika baa maarufu Mjini Dodoma ya Chako ni Chako baada ya Mmiliki wake kudaiwa kukiuka masharti ya kibali chake cha ujenzi.
Sehemu ya Baa Tango iliyopo eneo la Uhindini katikati ya Mji wa Dodoma nayo ilikumbwa na Bomoa Bomoa iliyoendeshwa na Manispaa ya Dodoma baada ya mmiliki wake kukiuka taratibu za ujenzi.
Sehemu ya Baa Tango iliyopo eneo la Uhindini katikati ya Mji wa Dodoma nayo ilikumbwa na Bomoa Bomoa iliyoendeshwa na Manispaa ya Dodoma baada ya mmiliki wake kukiuka taratibu za ujenzi.
Baadhi ya wasimamizi wa zoezi la bomoa bomoa (kulia) wakisaidia kutoa nje vifaa vya wapangaji wa nyumba iliyojengwa kwa kukiuka taratibu za ujenzi katika eneo la Kisasa jana kabla ya nyumba hiyo kubolewa wakati wa zoezi lililoendeshwa na Manispaa ya Dodoma.
Ubomoaji wa vibanda vilivyojengwa kando ya Barabara kuu ya Dodoma-Dar es Salaam ukiendelea wakati wa zoezi lililoendeshwa na Manispaa ya Dodoma jana.
Afisa Mdhibiti wa Ujenzi wa Manispaa ya Dodoma Ally Bellah akitoa ufafanuzi kwa Wanahabari juu ya zoezi la bomoa bomoa lililoendeshwa na Manispaa ya Dodoma jana.

.....................................

BAADHI ya Wakazi wa Manispaa ya Dodoma wameunga mkono zoezi la kubomoa nyumba na vibanda vilivyojengwa katika maeneo ya yasiyo rasmi ikiwemo hifadhi za barabara, maeneo ya wazi, na wale waliojenga katika viwanja wasivyovimiliki linalofanywa na Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma.

Baadhi ya wananchi waliotoa maoni yao katika maeneo ya Kisasa, Majengo, Nkuhungu, na Kikuyu ambapo zoezi hilo lilitekelezwa hapo jana, wamesema kumekuwapo na mazoea ya watu kuvamia maeneo yasiyo rasmi na kuanzisha makazi au vibanda vya biashara japo linaloharibu taswira ya Mji.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo la siku mbili lililoanza jana, Afisa Mdhibiti Ujenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Ally Bellah alisema zoezi hilo linafanyika kwa mujibu wa sheria na kwamba taratibu zote zimefuatwa kabla ya kufikia hatua ya uvunjaji.
“Maeneo yote haya tunayovunja wahusika walishapewa notisi kwa mujibu wa Sheria lakini wengi wao wamekaidi…kwa wale waliostahili kupewa fidia walishapewa fidia zao muda mrefu” alisema.
Bellah ametoa wito kwa Wakazi wote wa Manispaa ya hata wageni wanaohamia kuepuka kununua ardhi kienyeji kwani wanaweza kutapeliwa na kuuziwa maeneo ya wazi au yasiyo ya makazi na kujikuta wakipata usumbufu usio wa lazima.

“Hata wageni wanaohamia Manispaa ya Dodoma niseme kwamba tunawapenda sana na tunawakaribisha ila watakapohitaji ardhi au viwanja kwa ajili ya kujenga wahakikishe wanawasiliana na Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma ili wawe salama” alisistiza
Alisema Mji wa Dodoma ni Makao Makuu ya Nchi hivyo lazima uwe na muonekano wa kuvutia na kwamba zoezi la bomoa bomoa ni endelevu ili kudhibiti ujenzi holela na kusimamia ujenzi bora kwa mujibu wa vibali vinavyotolewa.
      

Wednesday, February 7, 2018

ZAIDI YA BILIONI 2.1 KUKARABATI BIHAWANA NA DODOMA SEKONDARI, WANAFUNZI WAIPONGEZA SERIKALI


Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Graceana Shirima (wa pili kushoto) akikagua shughuli ya ukarabati katika Shule ya Sekondari ya Dodoma baada ya kuzindua rasmi kazi hiyo. TEA imetoa zaidi ya Shilingi milioni 900 kwa ajili ya ukarabati huo. Kushoto ni Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi na kulia ni Mhandisi Lupakisyo Mwalwiba ambaye ni Meneja Miradi kutoka Chuo cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST)  ambaye ndiyo Mtaalamu Mshauri. PICHA: RAMADHANI JUMA-OFISI YA MKURUGENZI WA MANISPAA 
Kazi ya ukarabati ikiwa imeanza katika Shule ya Sekondari ya Dodoma
Kazi ya ukarabati ikiwa imeanza katika Shule ya Sekondari ya Dodoma
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TEA Graceana Shirima (wa pili kushoto) na Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (wa tatu kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja na wadau mbalimbali katika Shule ya Sekondari ya Dodoma baada ya kuzindua rasmi kazi ya ukarabati wa Shule hiyo jana.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TEA Graceana Shirima (kushoto) akikagua maeneo mbalimbali yanayofanyiwa ukarabati katika Shule ya Sekondari ya Bihawana iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma jana mara baada ya kufanya uzinduzi rasmi wa kazi hiyo. TEA imetoa zaidi ya Shilingi Bilioni 1.2 kwa ajili ya kuikarabati Shule hiyo.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TEA Graceana Shirima (wa nne kulia mbele) na muwakilishi wa Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma ambaye pia ni Afisa Elimu wa Manispaa hiyo Abdallah Membe (wa tano kulia mbele) wakiwa katika picha ya pamoja na wadau mbalimbali katika Shule ya Sekondari ya Bihawana baada ya kuzindua rasmi kazi ya ukarabati wa Shule hiyo jana.



..............................................

SERIKALI kupitia Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) imetoa zaidi ya shilingi Bilioni 2.1 kwa ajili ya kukarabati Shule za Sekondari za Bihawana na Dodoma zilizopo Manispaa ya Dodoma ikiwa ni sehemu ya utekezaji wa mpango wa Serikali wa kuzifanyia ukarabati mkubwa Shule kongwe Nchini.

Kati ya Fedha hizo, zaidi ya Shilingi Bilioni 1.2 zitatumika kukarabati Shule ya Sekondari ya Bihawana pekee na zaidi ya Shilingi Milioni 900 zitatumika katika Shule ya Sekondari ya Dodoma.

Akizungumza wakati wa uzinduzi rasmi wa kazi ya ukarabati katika shule hizo jana, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TEA Graceana Shirima alisema kuwa, shughuli ya ukarabati ilitanguliwa na upembuzi yakinifu wa hali halisi ya mahitaji ya ukarabati uliofanywa na mtaalamu mshauri ambaye ni Chuo cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST).

“Baada ya upembuzi yakinifu, maeneo ya kipaumbele katika ukarabati kwa awamu hii itahusisha Madarasa, maabara, bwalo na jiko,  vyoo, na mifumo ya umeme, mifumo ya TEHAMA na mifumo na maji safi na maji taka” alisema Shirima.

Alisema  awamu hii ya ukarabati inatarajiwa  kukamilika ndani ya kipindi cha  miezi minne, na awamu nyingine za ukarabati zitatekelezwa kulingana na upatikanaji wa fedha.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi aliishukuru Mamlaka ya Elimu kwa kuzipatia Shule za Manispaa hiyo Fedha nyingi kwa ajili ya ukarabati huku akitolea mfano wa Shule ya Wasichana ya Msalato ambayo ilishafanyiwa ukarabati mkubwa mwaka uliopita.

Kunambi aliahidi kuwa, Manispaa ya Dodoma  ambaye ndiye mmiliki wa Shule hizo itasimamia kwa karibu kila hatua ya kazi hiyo.

Baadhi ya Wanafunzi wa Shule zinazofanyiwa ukarabati wamepongeza hatua ya Serikali ya kutekeleza mpango huo na kwamba itawaboresha mazingira ya kujifunzia ikiwa ni pamoja na uimarishaji wa miundombinu muhimu kama umeme, maji, na mabweni.

Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia inatekeleza Mpango kabambe wa ukarabati wa Shule kongwe 89 za Sekondari Nchini ambao unafanyika kwa awamu.



Tuesday, February 6, 2018

MANISPAA YA DODOMA YAWEKA MKAKATI KUFAULISHA WOTE SHULE ZA MSINGI KUANZIA 2018


Mkuu wa Idara ya Elimu Msingi katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Mwikongi Kigosi (kushoto) akiwasilisha taarifa ya ya maendeleo ya Elimu kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dokta  Binilith Mahenge wakati wa ziara ya Mkuu huyo wa Mkoa katika Manispaa ya Dodoma hivi karibuni. 

 .................................

HALMASHAURI ya Manispaa ya Dodoma imeweka mkakati kabambe utakaowezesha kufikia lengo la ufaulu wa asilimia 100 kwa Wanafunzi wa Shule za Msingi kuanzia mwaka 2018.

Hayo yamebainishwa katika taarifa ya Manispaa hiyo iliyowasilishwa na Mkuu wa Idara ya Elimu Msingi Manispaa ya Dodoma Mwikongi Kigosi kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dokta Binilith Mahenge alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya Elimu na Afya hivi karibu katika Manispaa hiyo.

Kwa kujibu wa taarifa hiyo, miongoni mwa mikakati inayotarajiwa kutekelezwa ni pamoja na kuhakikisha wanafunzi wote wanamudu stadi za msingi za kusoma, kuandika na kuhesabu katika madarasa ya chini kabla ya kujiunga na madarasa yanayofuata.

Kigosi alisema mkakati mwingine ni kusimamia mahudhurio ya Walimu na Wanafunzi pamoja na kudhibiti matumizi ya simu kwa Walimu wawapo darasani.
Aidha, alisema Idara ya Elimu Msingi itateua shule 25 za serikali ambazo zitashindanishwa na shule za binafsi ili kubadilishana uzoefu na kuinua ufaulu katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma.

Vilevile alisema Idara imejipanga kuimarisha ufuatiliaji wa ufundishaji na kusimamia utendaji kazi wa walimu, sambamba na kutoa motisha kwa walimu na wanafunzi wanaofanya vizuri.

“Pia tutakuwa na mitihani, mazoezi na majaribio ya kufikirisha, pamoja na kambi za masomo… haya yote tutayafanya na tunaamini yatatupa matokeo tunayotarajia” alisema Kigosi.

Kwa mwaka 2017 jumla ya Wanafunzi 9,509  wakiwemo Wavulana 4,500 na Wasichana 5,009 walifanya mtihani wa kuhitimu Elimu ya Msingi katika Manispaa ya Dodoma ambapo Wanafunzi 6,488  wakiwemo Wavulana 3034 na Wasichana 3454 walifaulu, sawa na asilimia 68.

Friday, February 2, 2018

MKURUGENZI MANISPAA YA DODOMA AKABIDHI VITAMBULISHO KWA MMACHINGA 140


Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (wa pili kulia) akimvisha kitambulisho rasmi mmoja ya Wafanyabiashara ndogo wa soko la jioni katika eneo la viwanja vya Nyerere Mjini Dodoma wakati wa hafla ya kuwapatia vitambulisho wafanyabiashara hao iliyofanywa leo Februari 2, 2018. Jumla ya Wafanyabiashara 140 wa eneo hilo wamepatiwa vitambulisho hivyo. Kulia ni Ofisa Masoko wa Manispaa hiyo Steven Maufi.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (kushoto) akizungumza na Wafanyabiashara ndogo wa soko la jioni katika eneo la viwanja vya Nyerere Mjini Dodoma wakati wa hafla ya kuwapatia vitambulisho wafanyabiashara hao iliyofanywa leo Februari 2, 2018. Jumla ya Wafanyabiashara 140 wa eneo hilo wamepatiwa vitambulisho hivyo.
Baadhi ya Wafanyabiashara Ndogo wakifuatilia hotuba ya mgeni Rasmi
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (wa pili kulia) akimvisha kitambulisho rasmi mmoja ya Wafanyabiashara ndogo wa soko la jioni katika eneo la viwanja vya Nyerere Mjini Dodoma wakati wa hafla ya kuwapatia vitambulisho wafanyabiashara hao iliyofanywa leo Februari 2, 2018. Jumla ya Wafanyabiashara 140 wa eneo hilo wamepatiwa vitambulisho hivyo. Kulia ni Ofisa Masoko wa Manispaa hiyo Steven Maufi.

.....................................
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi amekabidhi vitambulisho kwa Wafanyabiashara ndogo maarufu kama m Machinga wanaofanya shughuli zao katika soko la jioni ili waweze kufahamiana wakati wa biashara zao na hata kusaidia kuimarisha masuala ya ulinzi  na usalama.

Wafanyabiashara ndogo wapatao 140 wanaofanya shughuli zao katika eneo la Viwanja vya Nyerere wamekabidhiwa vitambulisho hivyo na Mkurugenzi huyo katika hafla fupi iliyofanywa katika viwanja hivyo mchana wa leo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Kunambi amewaasa wafanyabiashara hao kuwa na utamaduni wa kutunza akiba ili kukuza mitaji yao huku akiwaahidi kuwaboreshea mazingira ya kazi zao na kwamba hakuna kiongozi atakayewaondoa katika maeneo hayo mpaka watakapatiwa maeneo mbadala na rafiki kwa biashara zao.

“Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. John Magufuli ni rafiki wa Machinga na ameshatoa maelekezo na nyinyi ni mashahidi…nawaahidi kusimamia maagizo ya Rais ya kuhakikisha wananchi wanyonge hawanyanyasiki ndani ya Nchi yao” alisema Kunambi.

Aliwataka wafanyabiashara kujiandaa kutumia fursa za ujenzi wa stendi mpya na ya kisasa na soko kubwa kwa ajili ya wafanyabiashara vitakavyojengwa katika Kata ya Nzuguni ili waweze kukua kibiashara.


“Tunaanza ujenzi wa stendi kubwa ya kisasa nay a mfano Afrika Mashariki na Kati katika eneo la Nzuguni Mwezi Machi 2018…ujenzi utakamilika baada ya miezi 24 na utaenda sambamba na ujenzi wa soko kubwa la kisasa kwahiyo jiandaeni kutumia hizo fursa” alisisitiza. 

Thursday, February 1, 2018

UJENZI WA STENDI KUBWA YA KISASA DODOMA KUANZA MACHI, NI YA KWANZA AFRIKA MASHARIKI


Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (kushoto) akizungumza wakati wa Mkutano wa Baraza la Madiwani lililofanyika jana Mjini hapa jana. Wa pili kushoto ni Meya wa Manispaa hiyo Mstahiki Profesa Davis Mwamfupe akiteta jambo na Naibu Meya Jumanne Ngede. Kulia ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Deo Ndejembi.
Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma wakifuatilia Mkutano wa Baraza hilo jana.
Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Deo Ndejembi akizungumza wakati wa Mkutano wa Baraza la Madiwani lililofanyika jana Mjini hapa jana.
Sehemu ya Wakuu wa Idara na Wageni waalikwa wakifuatilia Mkutano wa Baraza la Madiwani la  Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma wakifuatilia Mkutano wa Baraza hilo jana.
...................................................................

UJENZI wa stendi ya mabasi kubwa na ya kisasa  katika Manispaa ya Dodoma unatarajiwa kuanza mapema mwezi Machi mwaka huu katika eneo la Nzuguni nje kidogo ya Mji wa Dodoma.

Jumla ekari 50 zimetengwa katika eneo hilo lililopo mashariki mwa Mji barabra ya Dodoma-Dar es Salaam, ambapo ujenzi wa stendi hiyo unatarajiwa kukamilika baada ya kipindi cha miei 24.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi wakati wa mkutano wa Baraza la Madiwani lililofanyika Mjini hapa kwa ajili ya kupokea taarifa mbalimbali za kimaendeleo zilizotekelezwa katika kipindi cha robo ya pili ya mwaka wa Fedha 2018/2019 kinachoanzia Mwezi Septemba hadi Desemba 2018.


Kunambi aliwaambia wajumbe wa Mkutano huo kuwa, stendi hiyo ni kubwa na ya kisasa yenye hadhi ya Makao Makuu ya Nchi, na kwamba itakuwa ya mfano kwa Nchi zote za ukanda wa afrika Mashariki.

Friday, December 22, 2017

MKURUGENZI DODOMA KUWAKATIA BIMA YA AFYA 133 WANAOSAFISHA BARABARA MJINI, AWAPA ZAWADI YA KRISMASI NA MWAKA MPYA

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (kulia) akimkabidhi mche wa sabuni mmoja ya wafanyakazi wanaosafisha barabara na mitaa mbalimbali ya Mji wa Dodoma mara baada baada ya kuzungumza na wafanyakazi hao katika Viwanja vya Nyerere Mjini Dodoma jana. Mkurugenzi huyo aliwapatia wafanyakazi hao wapatao 133 zawadi ya Shilingi 10,000 na Mche mmoja wa sabuni kila mmoja ikiwa ni motisha hususan katika kipindi hiki cha Sikukuu za mwisho wa Mwaka.  PICHA: RAMADHANI JUMA-OFISI YA MKURUGENZI
Baadhi ya wafanyakazi wanaosafisha Barabara na Mitaa mbalimbali ya Mji wa Dodoma wakifurahia hotuba ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (hayupo pichani) wakati alipofanya nao mkutano katika Viwanja vya Nyerere Mjini Dodoma jana. 
 PICHA: RAMADHANI JUMA-OFISI YA MKURUGENZI

Mkuu wa Idara ya Mazingira na Usafishaji Manispaa ya Dodoma Dickson Kimaro (kushoto) akizungumza na wafanyakazi wanaosafisha barabara na mitaa mbalimbali ya Mji wa Dodoma kabla ya kumkaribisha Mkurugenzi wa Manispaa hiyo Godwin Kunambi (katikati) kuzungumza na wafanyakazi hao. kulia ni msimamizi wa wafanyakazi hao John Lugendo.


Wafanyakazi 133 wanaosafisha barabara na mitaa mbalimbali ya Mji wa Dodoma wakikabidhiwa Fedha taslim Shilingi 10,000 na mche wa sabuni kila mmoja ikiwa ni zawadi ya motisha iliyotolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (hayupo pichani) jana katika Viwanja vya Nerere Mjini Dodoma. Wanaokabidhi ni Mkuu wa Idara ya Mazingira na Usafishaji Manispaa ya Dodoma Dickson Kimaro (wa pili waliokaa) na Afisa Mazingira ambaye ni Msimamzi wa Wafanyakazi hao John Lugendo (wa kwanza waliokaa). PICHA: RAMADHANI JUMA-OFISI YA MKURUGENZI
Sehemu ya wafanyakazi wanaosafisha Barabara na Mitaa mbalimbali ya Mji wa Dodoma wakifuatilia hotuba ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi (hayupo pichani) wakati alipofanya nao mkutano katika Viwanja vya Nyerere Mjini Dodoma jana. Kando ni maboksi ya sabuni ambapo kila mmoja alizawadia mche mmoja na fedha taslimu Shilingi 10,000 na Mkurugenzi huyo huku akiwaahidi kuwakatia Bima ya Afya.  PICHA: RAMADHANI JUMA-OFISI YA MKURUGENZI

.....................................................

MKURUGENZI wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma Godwin Kunambi ameahidi kuwakatia Bima ya Afya wafanyakazi 133 wanaosafisha mitaa na barabara zote za Mji wa Dodoma ili wawe na uhakika wa matibabu wao na familia zao.

Alitoa ahadi hiyo jana alipofanya mkutano na wafanyakazi hao katika viwanja vya Nyerere katikati ya Mji wa Dodoma ambapo pia aliwapatia fedha taslimu Shilingi 10,000 na mche mmoja wa sabuni kila mmoja kama zawadi kuelekea mwisho wa mwaka 2017.

Mkurugenzi Kunambi alisema kuwa, yeye kwa niaba ya Uongozi wa Manispaa  ametoa zawadi na ahadi ya kuwakatia Bima ya matibabu baada ya kufurahishwa na uchapa kazi wao unaopelekea mitaa na barabara za Mji kuwa safi na kupendeza muda wote.

“Hiki tunachowapa leo hakina thamani yeyote kwa kazi kubwa mnayoifanya, bali ni kuonesha kuguswa kwetu tu kama Manispaa…ninyi ni kundi maalum na ni wafanyakazi muhimu sana” alisema Kunambi akizungumza na watumishi hao.

“Nimefurahi kukutana na kuzungumza na ninyi kipindi hiki cha mwisho wa mwaka…nawaahidi mapema mwakani Manispaa itawakatika Bima za Afya wote itakayomwawezesha kila mmoja kutibiwa yeye na wategemezi wake watatu” alifafanua.

Kwa upande wao, wafanyakazi hao ambao wengi wao ni akina Mama walimshukuru Mkurugenzi huyo kwa niaba ya Manispaa kwa kuwajali licha ya kuwa wao ni watumishi wa kada ya chini na wanaofanya kazi kwa mkataba isiyo ya kudumu.

“Tumefurahi sana leo Mkurugenzi wetu umekuja kuongea na sisi na kutupa zawadi na fedha tena katika kipindi cha Sikukuu za mwisho wa mwaka...umetujali sana na sisi tunakuombea kwa Mugu”… alisema mmoja ya akia mama hao akimshukuru Mkurugenzi wa Manispaa.