.......................................
MKUU wa Mkoa wa Dodoma
Dokta Binilith Mahenge amewataka watumishi na viongozi wa Halmashauri Mkoani humo
kuhakikisha wanayapa kipaumbele mambo
matano ikiwemo kudumisha hali ya Ulinzi na Usalama ambayo ndiyo nguzo muhimu inayopelekea shughuli nyingine za maendeleo
kufanyika kwa ufanisi ili kuifanya Dodoma ikue kwa kasi.
Mambo mengine aliyoyayaorodhesha
Mkuu huyo wa Mkoa kama dira ya kuharakisha maendeleo ni pamoja na utayari wa
kubadilika kwa watumishi na kutofanya kazi kwa mazoea, utoaji wa huduma bora na
zenye viwango kwa wananchi, kudumisha dhana ya Ushirikishwaji baina ya Taasisi
na miongoni mwa watumishi, na kuepuka migogoro baina ya watumishi ndani ya
Taasisi hali inayoweza kudumaza malengo ya Serikali katika kuwadumia wananchi.
Mkuu wa Mkoa Mahenge
aliyasema hayo wakati alipokuwa akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya
Manispaa ya Dodoma alipofanya ziara ya kujitambulisha katika Wilaya ya Dodoma
Novemba 24 mwaka huu.
Awali alipokea taarifa ya
maendeleo ya Wilaya iliyowasilishwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya
Dodoma Godwin Kunambi kwa niaba ya Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma ambaye pia ni
Mkuu wa Wilaya ya Chamwino Vumilia Nyamoga.
